2015-02-13 09:01:08

Chuki za kidini!


Mapambano dhidi ya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram nchini Nigeria pamoja na sakata la vikatuni vya kashfa dhidi ya dini ya Kiislam, ni mambo ambayo yanachangia uwepo wa hali tete ya mahusiano kati ya waamini wa dini ya Kiislam na Kikristo nchini Niger. Hali hii ilipelekea hivi karibuni, Makanisa kadhaa kuchomwa moto kwa kisingizio cha misimamo mikali ya kidini.

Uamuzi uliofanywa na Serikali ya Niger ya kuunga mkono mapambano dhidi ya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram kutoka Nigeria yametibua tena nyongo za waamini wa dini ya Kiislam nchini Niger kwa kisingizio kwamba, haya ni mashambulizi dhidi ya Kikundi kinachotetea misingi ya dini ya Kiislam, jambo ambalo si kweli kabisa!

Kwa sasa Nchi za Afrika Magharibi, yaani: Nigeria, Cameroon, Chad na Benin, zimeamua kuunganisha nguvu zao dhidi ya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram na cheche za matumaini zinaanza kuonekana, ingawa Boko Haram kinaendelea kusababisha maafa makubwa zaidi kwa watu na mali zao. Vijana wengi wanaajiriwa kwenye makundi ya kigaidi kutokana na ukosefu wa ajira, unaowasababishia ukata mkubwa pamoja na kukosa dira na mwelekeo wa maisha.

Mashuhuda wanasema, ni vijana hawa ndio waliohusika katika matukio ya kuchomwa moto kwa makanisa nchini Niger hivi karibuni. Itakumbukwa kwamba, tukio kama hili la vijana wenye misimamo mikali ya kidini, liliwahi kutokea kunako mwaka 2012. Matukio yote haya ni cheche dhidi ya Wakristo huko Niger, jambo ambalo ni tishio kwa usalama na maisha ya watu; uhuru wa kuabudu; utu na heshima ya binadamu.

Kanisa linapenda kujielekeza zaidi katika majadiliano yanayojikita katika uhalisia wa maisha kwa kusaidiana, kuheshimiana na kupendana kama watu wa jamii moja, ili kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa na kwamba, dini kisiwe ni chanzo cha vurugu, kinzani na misigano ya kijamii, kwani wanaoumia ni wanyonge ndani ya jamii. Wanasiasa wakati mwingine wamekuwa ni chachu ya vurugu za kidini kwa ajili ya masilahi binafsi, jambo ambalo ni hatari kabisa kwa mfungamano na mshikamano wa kitaifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.