2015-02-12 07:46:25

Makardinali waanza mkutano mjini Vatican


Baraza la Makardinali Washauri kuhusu mabadiliko ya Sekretarieti ya limehitimisha kikao chake cha tisa kwa ushiriki wa Baba Mtakatifu Francisko. Makardinali hawa watakutana tena kuanzia tarehe 13 hadi 15 Aprili 2015. Hayo yamebainishwa na Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican wakati akizungumza na waandishi wa Habari mjini Vatican siku ya Jumatano, tarehe 11 Februari 2015.

Kwa sasa kuna Waraka ambao unaendelea kuandaliwa ambao kimsingi unahitaji muda mrefu, kwani hii itakuwa ni Katiba mpya na wala si tu marekebisho ya nyaraka zilizokwishawahi kutolewa kuhusu Sekretarieti ya Vatican. Kikao cha mwisho kimeandaa taarifa kwa ajili ya kikao cha Makardinali wote ambacho kinaanza, Alhamisi, tarehe 12 Februari 2015 na utangulizi wake unatolewa na Kardinali Rodriguez Maradiaga.

Baraza la Makardinali limefafanuliwa kuhusu: kazi, majukumu na maendeleo yaliyokwishafikiwa na Sekretarieti pamoja na Baraza la Kipapa la Uchumi. Wamesikiliza pia taarifa ya Tume ya Kipapa ya kulinda watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia. Alhamisi, Makardinali wote wanafanya kikao ambacho kinatanguliwa na taarifa elekezi kutoka kwa Baraza la Makardinali na baadaye Makardinali wataanza kuchangia maoni yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.