2015-02-12 11:45:24

Lengo ni ufanisi na ubora wa kazi!


Tazama inavyopendeza ndugu kukaa kwa pamoja katika umoja na mapendo, lakini kwa namna ya pekee wakati huu, Kanisa linapowakaribisha Makardinali wateule 20, kwa pamoja kuweza kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa Kikanisa. Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko kwa Makardinali walioanza mkutano wao wa kawaida mjini Vatican, Alhamisi, tarehe 12 Februari 2015.

Baba Mtakatifu anawashukuru viongozi wote wa Kanisa walioandaa tukio hili muhimu katika maisha na utume wa Kanisa, kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya muswada wa Waraka unaopania kufanya mageuzi makubwa katika Sekretarieti ya Vatican. Huu ni muhtasari wa mchango wa mawazo kutoka kutoka kwa wakuu wa Mabaraza ya Kipapa na wataalam katika sekta husika, lengo ni kuleta maboresho ya kazi zinazotekelezwa na Sekretarieti ya Vatican, ili kuongeza tija na ufanisi; ukweli na uwazi; mambo msingi yanayojenga na kuimarisha mwono wa kisinodi na mshikamano wa kikanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, lengo la mabadiliko yanayofanyiwa kazi kwa sasa ni kuliwezesha Kanisa kuwa shuhuda makini, ili kusaidia mchakato wa maboresho katika azma ya Uinjilishaji; kukuza na kuimarisha majadiliano ya kiekumene na kidini; changamoto iliyotolewa na Makardinali katika mikutano yao elekezi. Sekretarieti ya Vatican inapaswa kuboreshwa zaidi, ili kutoa utambulisho wenye mvuto na maguso pamoja na kuendelea kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara. Lengo kuu ni kuimarisha umoja katika imani, upendo na mshikamano kati ya watu wa Mungu na kuendeleza utume wa Kanisa ulimwenguni.

Baba Mtakatifu anakiri kwamba, hapa kuna kazi pevu, ili kuweza kufikia lengo, kwani kunahitajika muda, ari, lakini zaidi ushirikiano na wadau mbali mbali sanjari na kuendelea kumwomba Roho Mtakatifu, aliongoze Kanisa, katika maamuzi na mang'amuzi yake. Mkutano huu utaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa anasema Baba Mtakatifu, ikiwa kama kila Kardinali atachangia mawazo pamoja na kuendelea kuwa waaminifu kwa Mafundisho ya Kanisa, kwa ajili ya amani na ustawi wa roho za waamini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.