2015-02-12 12:16:12

Lengo ni kushirikisha uzoefu na mang'amuzi!


Tukio la Makardinali kukusanyika kumzunguka Khalifa wa Mtakatifu Petro, chini ya usimamizi na uongozi wa Roho Mtakatifu, ni kielelezo cha imani na utashi wa kutaka kushirikiana na Baba Mtakatifu kwa karibu zaidi, ili kumwezesha kutekeleza dhamana na utume wake kwa uaminifu na tija zaidi.

Makardinali wa Kanisa Katoliki wanayo nafasi muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa, kwani wao ni washauri wakuu kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro katika utekelezaji wa dhamana yake kama kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki. Hizi ni salam na matashi mema yaliyotolewa na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Makardinali mjini Vatican, siku ya Alhamisi, tarehe 12 Februari 2015 na kukazia kwamba, Makardinali kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanapenda kushirikisha mawazo, uzoefu na manga'muzi yao kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Kardinali Sodano anasema kuna jumla ya Makardinali 228, lakini hawakuweza kuhudhuria wote kutokana na umri, ugonjwa na bila kumsahau Kardinali Karl Joseph Becker, SJ, aliyefariki dunia hivi karibuni na anatarajiwa kusindikizwa katika usingizi wa milele katika Ibada ya Misa Takatifu itakayoongozwa na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali, Jumatatu, tarehe 16 Februari 2015, majira ya saa 8. 45 mchana kwa Saa za Ulaya. Baba Mtakatifu atahitimisha sala kwa Ibada ya Maziko. Ibada hii itafanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican.

Kardinali Sodano anasema, wanapenda kuchangia mchakato wa mageuzi makubwa yanayotarajiwa kufanywa na Mama Kanisa katika Katiba ya Kitume, Mchungaji Mwema, "Pastor Bonus", matunda ya marekebisho ya Nyaraka mbali mbali zilizotungwa na Papa Pio wa Kumi, Mwenyeheri Paulo VI na Mtakatifu Yohane Paulo II, walioleta muundo wa Sekretarieti ya Vatican kama ulivyo kwa sasa. Lengo ni kusoma alama za nyakati, ili kulisaidia Kanisa kukabiliana na changamoto katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo na kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.