2015-02-12 08:31:32

Hayo ni mauaji na wala si huruma kwa wagonjwa!


Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji, kuwasaidia wagonjwa, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, lakini kwa namna ya pekee kabisa kuwaonjesha huruma na mapendo, wagonjwa walioko kufani! Hiki ndicho kielelezo makini cha huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linabainisha kwamba, kumsaidia mgonjwa kupata kifo laini si tendo na huruma, haki wala uungwana bali ni mauaji ya kikatili, kwani maisha ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayopaswa kulindwa na kuheshimiwa na wote. Hukumu iliyotolewa na Mahakama kuu ya Canada hivi karibuni kwamba, madaktari wanaweza kuwasaidia wagonjwa walioko kufani au wenye magonjwa yasiyokuwa na tiba kupata kifo laini, ni hukumu inayokwenda kinyume na utu na haki msingi za binadamu, kwani kila mtu anayo haki ya kuishi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwasaidia na kuwafariji wagonjwa, ili asiwepo kamwe mgonjwa ambaye atakumbwa na upweke kiasi hata cha kujikatia tamaa ya maisha na kutamani kupata kifo laini. Baraza la Maaskofu kwa upande wake, litaendelea kuwasaidia wagonjwa kupata matibabu msingi pamoja na kuwasaidia wagonjwa wa walioko majumbani; wazee na walemavu, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu.

Maaskofu wanaishauri Serikali kufuta hukumu hii inayoonekana kuwa na huruma kwa wagonjwa lakini ndani mwake, inafumbata utamaduni wa kifo, changamoto kwa viongozi wa Serikali kuhakikisha kwamba, wanatoa huduma bora na makini kwa wananchi wao; wanawataka mawakala wa Serikali na wanataaluma kuibua sera na mikakati inayoheshimu uhuru wa dhamiri kwa wafanyakazi wote na kwamba, mauaji hayawezi kukubalika kwa kisingizio cha huruma kwa wagonjwa dhidi ya mateso na mahangaiko yao.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.