2015-02-11 08:53:59

Msiwakejeli wagonjwa!


Monsinyo Jean Marie Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, katika maadhimisho ya Siku ya ishirini na tatu ya wagonjwa duniani kwa mwaka 2015 anasema, kuna uhusiano mkubwa kati mgonjwa, mhudumu na jamaa kwani wote kwa pamoja wanafanya hija ya maisha inayojikita katika hekima ya moyo. Siku hii inaongozwa na kauli mbiu "Nalikuwa macho kwa kipofu, nalikuwa mguu kwa aliyechechemea".

Mahusiano kati ya mgonjwa na mhudumu wa afya ni mkutano ambao unajenga na kuimarisha imani ambayo mgonjwa anaijenga kwa daktari na utambuzi ambao daktari anaudhihirisha kwa mgonjwa kutokana na taaluma yake na kwamba, Kanisa hapa linatambua kuwa hii ni huduma inayolenga kudumisha Injili ya Uhai. Tiba pamoja na mambo mengine haina budi kuzingatia maisha ya mtu: kimwili, kiroho na kisaikolojia, hapa hekima ya moyoni haina budi kuzingatiwa kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko.

Wahudumu wa sekta ya afya wawaone wagonjwa kuwa kama ndugu zao, ili kweli huduma wanayoitoa iwe ni ushuhuda wa faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu na mahali pa kutangaza uwepo wa Ufalme wa Mungu. Huduma kwa wagonjwa ni hija ya kuutafuta utakatifu wa maisha; fursa ya kukuza na kuimarisha imani, matumaini na mapendo sanjari na kutangaza Injili ya Uhai, kwa njia ya huduma makini. Wahudumu wa sekta ya afya wanaalikwa kuwa kweli ni Wasamaria wema wanaowaganga wagonjwa kwa mafuta ya upendo na huruma inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Huu ni mwaliko wa kujenga na kudumisha utamaduni wa upendo na mshikamano wa kidugu katika ulimwengu wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu; kwa kutambua kwamba, kila tendo wanalolitenda kwa ajili ya wagonjwa wanamtendea Kristo anayejifananisha na watu kama hawa. Wagonjwa na wote wanaoteseka: kiroho na kimwili ni hazina kubwa katika maisha na utume wa Kanisa; wanayo heshima na utu wao kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Wagonjwa waonjeshwe, urafiki na udugu wa kweli bila kuwakejeli wala kuwadhihaki. Mgonjwa ana hamu ya maisha na anashiriki kikamilifu katika asili ya mwanadamu na kwamba, anahitaji kuonjeshwa upendo na huruma; mambo ambayo yanajikita anasema Monsinyo Mupendawatu katika toba na wongofu wa ndani!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.