2015-02-11 12:15:56

Mheshimiwa Padre Ernest Ngboko Ngombe ateuliwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Lisala, DRC


Baba Mtakatifu Francisko amekubali ombi lililowasilishwa kwake na Askofu Louis Nkinga Bondala wa Jimbo Katoliki la Lisala lililoko nchini DRC ili kung'atuka kutoka madarakani. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Mheshimiwa Padre Ernest Ngboko Ngombe, C.I.C.M, Makamu mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Scheut kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Lisala.

Askofu mteule Ernest Ngboko Ngombe alizaiwa tarehe 25 Mei 1964 Jimboni Lisala baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa nchini Cameroon, aliweka nadhiri zake za kwanza kwenye Shirika hapo tarehe 17 Oktoba 1987 na baadaye kupadrishwa tarehe 20 Juni 1996 huko Dakar, Senegal.

Tangu wakati huo katika maisha na utume wake kama Padre amekuwa Paroko msaidizi, Mkuu wa Shirika mahalia na kuanzia mwaka 2001 hadi mwaka 2011 alipelekwa kujiendeleza kwa masomo ya juu katika masuala ya kitaalimungu na kujipatia Shahada ya Uzamili kutoka katika Chuo Kikuu cha Catholic Theological Union, kilichoko nchini Marekani.

Kunako mwaka 2011 aliteuliwa kuwa ni Gombera wa Seminari kuu ya Kitaalimungu iliyoko nchini Cameroon na Mratibu wa Shirika, Kanda ya Afrika. Kunako mwaka 2011 hadi kuteuliwa kwake kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Lisala, amekuwa ni Makamu mkuu wa Shirika na makazi yake yakiwa mjini Roma.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.