2015-02-10 09:22:17

Shukrani SDA kwa kuwekeza kwa vijana


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amelisifu Kanisa la Seventh Day Adventist (SDA) duniani kwa kujali na kushughulikia matatizo ya vijana akisema kuwa vijana wa kizazi kipya wanapitia katika dunia ngumu zaidi na majaribu makubwa zaidi kuliko marika yaliyowatangulia.

“Nimefurahi na nawapongeza kuwa pia mliangalia matatizo ya vijana katika mkutano wetu wa Dar es salaam kwa sababu vijana wetu wanapitia katika dunia ngumu zaidi na majaribu makubwa zaidi kuliko yale ambayo sisi wazazi wao tulipitia,” Rais Kikwete aliuambia uongozi wa SDA ukiongozwa na Kiongozi Mkuu wa Kanisa hilo duniani, Dkt. Ted N.C. Wilson na kuongeza: “Vijana wetu sasa wanakabiliwa na mifumo ya kisasa zaidi ya mawasiliano duniani ambayo inawalazimisha kukabiliana na majaribu mengi – televisheni imekuwa ya dunia nzima (global), intaneti sasa imekuwa ya dunia nzima na mitandao ya mawasiliano ya kijamii imekuwa ya dunia nzima na kila kimoja kinashusha aina yake ya habari kwa vijana wetu.”

Pongezi hizo kwa SDA zilitolewa mwishoni mwa wiki, Jumamosi, Februari 7, 2015, na Rais Kikwete wakati wa chakula cha jioni ambacho aliwaandalia viongozi hao wa SDA kutoka sehemu mbali mbali duniani, zikiwemo nchi 11 za Afrika, wakiongozwa na Dkt. Wilson ambaye ni Kiongozi Mkuu wa SDA na Rais wa the General Conference of the Seventh Adventist Church.

Dkt. Wilson na viongozi wa SDA kutoka nchi mbali mbali duniani walikuwa nchini kushiriki katika mkutano wa kidini ujulikanao kama Blessings in Mission East and Central Africa ambao ulifanyika Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa mjini Dar Es Salaam. Dkt. Wilson alimweleza Rais Kikwete kuwa Kanisa lake limefanya mkutano mzuri na wa kuvutia na kuwa inakadiriwa kuwa kiasi cha watu 40,000 kutoka ndani na nje ya Tanzania walishiriki mkutano huo.








All the contents on this site are copyrighted ©.