2015-02-10 15:15:04

Kardinali Karl Joseph Becker amefariki dunia!


Baba Mtakatifu Francisko amepokea taarifa ya msiba wa Kardinali Karl Joseph Becker kutoka Shirika la Wayesuit, aliyefariki dunia, tarehe 10 Februari 2015 kwa majonzi makubwa na amemtumia salam za rambi rambi Mheshimiwa Padre Adolfo NIcolàs Pachon, Mkuu wa Shirika la Wayesuit, kwa kumkumbuka Kardinali Becker kwa sadaka na majitoleo yake katika maisha na utume wa Kanisa.

Ni kiongozi alijipambanua kwa kuwafunda vijana wa kizazi kipya, hususan mapadre katika tafiti za kitaalimungu pamoja na huduma kwa Kanisa la Kiulimwengu. Baba Mtakatifu anamwomba Bikira Maria na kwa maombezi ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola, waweze kumwombea Marehemu Kardinali Becker, ili aweze kupokelewa katika maisha ya uzima wa milele.

Kardinali Becker alizaliwa kunako mwaka 1928, nchini Ujerumani, akajiunga na Shirika la Wayesuit akiwa na umri wa miaka ishirini. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akadrishwa kunako mwaka 1958. Kwa miaka mingi amekuwa ni jaalim la Mafundisho tanzu ya Kanisa, huko Frankfurt na katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian, kilichoko mjini Roma. Alikuwa ni mjumbe wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa. Kunako tarehe 18 Februari 2012 aliteuliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kuwa Kardinali, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 86.

Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anaungana na wote wanaoomboleza kifo cha kardinali Becker, aliyependwa na kuheshimiwa sana na vijana wa kizazi kipya, kutokana na hekima na umahiri wake katika kufundisha; anamwombea maisha ya uzima wa milele.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.