2015-02-09 11:31:10

Utunzaji bora wa mazingira!


Wakristo pamoja na watu wote wenye mapenzi mema wanahamasishwa kulinda na kutunza mazingira ambayo kwa namna ya pekee kabisa yamepyaishwa na Kristo, kwa kumwondoa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti; kwa kuwaponywa watu na magonjwa yao na hivyo kuwapatia tena maisha mapya. Yesu katika maisha na utume wake alikuwa anakutana na watu; wagonjwa walipomgusa mavazi yake wakaponywa na mateso pamoja na mahangaiko yao, changamoto na mwaliko kwa waamini kudumu katika imani, kazi inayotekelezwa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumatatu, tarehe 9 Februari 2015 anasema kwamba, Mwenyezi Mungu anaendelea kuumba, kazi inayobubujika kutoka katika upendo wake na kwamba, mwanadamu anawajibika kulinda na kutunza mazingira, kwani amekabidhiwa dhamana hii na wala si mmiliki wa kazi ya uumbaji.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kwa namna ya pekee kuhakikisha kwamba, wanashiriki katika kulinda na kutunza mazingira mintarafu sheria za nchi na wala si wajibu wa wakereketwa wa utunzaji wa mazingira, ili kuendeleza kazi ya uumbaji pamoja na kujiachilia mikononi mwa Kristo ili aweze kuwapatanisha, katika ngazi ya mtu binafsi, katika jumuiya pamoja na kuwapatanisha na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Yesu Kristo. Waamini wanapaswa kukumbuka kwamba, Roho Mtakatifu anatenda kazi ndani mwao, ili kukua na kukomaa katika imani, matumaini na mapendo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.