2015-02-09 09:29:15

Lindeni watoto!


Tume ya Kipapa kwa ajili ya ulinzi kwa watoto imehitimisha mkutano wake wa kwanza uliokuwa unafanyika mjini Vatican chini ya uongozi wa Kardinali Sèan Patrick O’Malley, Rais wa tume hii aliyewataka viongozi mbali mbali wa Kanisa kushirikiana na tume, ili kuwalinda, kuwatetea na kuwaendeleza watoto dhidi ya nyanyaso za kijinsia, kwa kufungua ukurasa mpya wa upatanisho na uponyaji kwa wale wote walioguswa na mkasa huu.

Ni mwaliko kwa viongozi wa Kanisa kama anavyosisitizia Baba Mtakatifu kuhakikisha kwamba, wanaunda mazingira yatakayowahakikishia watoto usalama wa maisha yao sanjari na viongozi hawa kukutana, kuzungumza, kuwasaidia pamoja na kuomba msamaha. Mambo ambayo yamepewa mkazo wa pekee na Baba Mtakatifu Francisko katika barua yake kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki ulimwenguni na kwa wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Ni wajibu wa Mabaraza ya Maaskofu kuunda tume itakayobainisha dira na mwongozo wa kupambana na nyanyaso za kijinsia.

Tume hii itakuwa inashirikiana na Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa, itakayotoa mwongozo na suluhu makini ya kukabiliana na matatizo kama haya yanapojitokeza. Ni jukumu la Tume hii kuandaa sera na mikakati ya elimu na majiundo makini itakayokuwa na programu na mbinu za kuwalinda watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia.

Kardinali Sèan Patrick O’Malley anasema, kwa mara ya kwanza katika mkutano wa Tume ya Kipapa kwa ajili ya ulinzi kwa watoto, wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia walioteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko wameshiriki kwa ukamilifu kwa kuchangia mawazo, uzoefu na mang’amuzi yao katika mchakato wa mapambano dhidi ya nyanyaso za kijinsia kwa watoto wadogo.

Tume kwa sasa inaandaa semina ili kuwajengea uwezo viongozi wa Kanisa katika mikakati ya kuwalinda watoto; semina zitakazotolewa kwa viongozi wa Sekretarieti ya Vatican pamoja na Maaskofu wapya wanaofika mjini Vatican kila mwaka kwa ajili ya kupata semina elekezi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu majimboni mwao.

Tume inaendelea kuandaa vitini kwa ajili ya sala kwa watu walioguswa na mkasa huu katika maisha yao kama sehemu ya mchakato wa uponyaji wa maisha ya kiroho pamoja na kuhamasisha waamini kutambua madhara na athari za nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo.

Tume pia inaanza kutafuta fedha kutoka kwa Mashirika mbali mbali ya misaada ili kuwasaidia waathirika wa nyanyaso za kijinsia pamoja na mafunzo. Tume inapania kushirikiana na waathirika wa nyanyaso za kijinsia ili kusaidia kutoa mawazo ya kuwakinga watoto pamoja na miongozo makini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.