Kusoma, Kuandika na Kuhesabu vyawekewa mkakati maalum!
Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amezindua Mpango wa Kitaifa wa Kukuza Stadi
za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) unaolenga kukuza viwango vya uelewa kwa watoto
wa darasa la kwanza na la pili nchini Tanzania. Mpango huo wa miaka mitatu ulioanza
kutekelezwa 2014/2015 hadi 2016/2017 umelengwa kuwahusisha watoto wenye umri wa miaka
mitano hadi 13 walio kwenye mfumo rasmi wa elimu na usio rasmi (MEMKWA).
Akizungumza
na wadau wa elimu, walimu na wanafunzi walioshiriki uzinduzi huo Jumamosi, Februari
7, 2015, Waziri Mkuu Pinda alisema mpango huo ni mkubwa na umeandaliwa mahsusi kujibu
changamoto zilizojitokeza miaka ya nyuma. Aliwataka watekelezaji wakuu wa mpango ambao
ni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) pamoja na
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kuhakikisha kuwa wanazishirikisha asasi
zisizo za Kiserikali ambazo zinajihusisha na masuala ya elimu.
“Kuna mashirika
mengi yasiyo za kiserikali ambayo ni chachu ya kuhimiza elimu nchini... jaribuni kuwashirikisha
sababu wao ni wadau wazuri sana wa suala hili. Pangeni utaratibu wa kukaa na hawa
wadau na kuwapa mrejesho wa mpango huu mzima,”alisema Waziri Mkuu.
Hata hivyo,
Waziri Mkuu aliwataka wahusika wakuu wa mpango waangalie mgawanyo wa mikoa iliyoingizwa
kwenye mpango huo kwa kuzingatia kanda ili kuleta matokeo ya mtawanyiko badala ya
hali ilivyo sasa. “Nimeangalia jinsi mlivyogawa mikoa yenu, inanipa taabu kidogo...
kuna mikoa inahitaji msukumo wa pekee, mikoa ya wadugaji, mikoa iliyoko pwani ya bahari
na maziwa, yote inahitaji msukumo wa tofauti,” alisema.
Katika taarifa yao,
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ilisema mpango huo wa KKK au LANES (Literacy
and Numeracy Support Programme) unafadhiliwa na Ushirika wa Kimataifa wa Maendeleo
ya Elimu (Global Partnership for Education – GPE) na wahisani wengine. Wahisani
hao ni pamoja na Shirika la Maendeleo la Uingereza (DFID) kupitia mradi wa EQUIP-T
unaotekelezwa katika mikoa saba ya Kigoma, Shinyanga, Mara, Simiyu, Lindi, Dodoma
na Tabora; Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Elimu kwa Mtoto (UNICEF) wanaofadhili
utelekezaji wa Mpango wa LANES katika mikoa ya Iringa, Mbeya na Njombe; na Shirika
la Maendeleo la Marekani (USAID) kupitia Mradi wa TZ-21 unaotekelezwa katika mkoa
wa Mtwara. Mapema, akisoma taarifa ya mpango huo mbele ya Waziri Mkuu, Kamishna
wa Elimu nchini, Prof. Eustella Bhalalusesa alisema mpango huo umelenga kuongeza ufanisi
katika stadi za KKK, kurahisisha kazi ya walimu wanaofundisha watoto wa darasa la
kwanza na la pili pamoja na kuongeza ushiriki wa jamii katika kuboresha elimu na hasa
ujifunzaji wa stadi za KKK. Alisema mpango huo utachangiwa sh. bilioni 150 ambazo
zitaingizwa moja kwa moja kwenye mfuko wa elimu kupitia Wizara ya Fedha. Alisema
maandalizi yote ya utekelezaji wa mpango huu yamekamilika ikiwa ni pamoja na mtaala
wa darasa la kwanza na darasa la pili, muhtasari wa KKK kwa darasa la I & II, pamoja
na Mwongozo wa Mwalimu wa kufundisha kusoma kuandika na kuhesabu.