2015-02-09 09:45:15

Changamoto za familia!


Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu, hivi karibuni akiwa mjini Nazareth amewashirikisha viongozi wakuu wa Kanisa kutoka Nchi Takatifu pamoja na familia kuhusu maendeleo ya maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia inayotarajiwa kufanyika mjini Vatican mwezi Oktoba, 2015.
Familia zinazoishi katika Nchi Takatifu zinahitaji kujikita katika fadhila ya matumaini kwani zinakabiliwa na matatizo pamoja na changamoto mbali mbali kama zilivyofafanuliwa na viongozi wa Kanisa wakati wanashirikisha mawazo, tafakari na maoni katika kongamano hili lililoandaliwa kama sehemu ya mwendelezo wa maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia iliyofanyikwa mjini Vatican kunako mwaka 2014.
Matatizo na changamoto za kisiasa na kiuchumi; ukosefu wa amani, usalama na utulivu; ukosefu wa fursa za ajira; changamoto za malezi kwa watoto wanaozaliwa katika ndoa mseto; tatizo la wahamiaji; changamoto na athari za mitandao ya kijamii katika tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Kuna changamoto za majadiliano ya kiekumene katika masuala ya kifamilia kwa waamini wanaohamia kwenye Makanisa mengine ya Kikristo; tatizo la kushiriki kikamilifu katika maisha ya Kisakramenti: hususan Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na ile ya Upatanisho. Bado kuna ukiritimba wa kupata haki kwa wanandoa ambao wanakabiliwa na mashaka ya uhalali wa ndoa zao.
Kardinali Baldisseri anabainisha kwamba, hati ya Mababa wa Sinodi ya Maaskofu iliyohitimishwa mwaka 2014 inapembua kwa kina na mapana mada mbali mbali zilizowasilishwa katika kongamano hili mintarafu hali halisi ya maisha ya ndoa na familia huko Mashariki ya Kati. Hati hii imekuwa ni sehemu ya mwongozo uliotumwa kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki, ili uweze kujadiliwa, tayari kuanza mchakato wa Hati ya Kutendea Kazi, yaani, “Instrumentum Laboris”.
Mang’amuzi ya maadhimisho ya Sinodi maalum kwa ajili ya familia, lilikuwa ni tukio la neema na baraka kwa maisha na utume wa Kanisa, kama alivyofafanua Baba Mtakatifu Francisko. Mababa wa Sinodi walitambua na kuguswa na matumaini, matatizo, changamoto na fursa mbali mbali zinazozikabili familia. Mababa wa Sinodi walimshukuru Mungu kwa uaminifu unaotekelezwa na familia nyingi katika maisha na utume wao kama familia za Kikristo, licha ya matatizo, changamoto na vikwazo vinavyoendelea kujitokeza mbele yao.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.