Kuna haja ya kuthamini tofauti zinazojitokeza katika maisha ya mwanadamu, ili kujenga
na kudumisha umoja na mshikamano wa dhati na kwamba, hakuna mabadiliko ya kweli yanayoweza
kufanywa katika maisha ya binadamu bila kuzingatia elimu! Mabadiliko katika mfumo
wa elimu ni kikolezo kikuu cha maendeleo ya mwanadamu sehemu mbali mbali za dunia.
Hapa kuna haja ya kuimarisha ushirikiano kati ya familia, shule, jamii na
tamaduni za watu, ili kuleta mabadiliko yanayokusudiwa katika maisha ya mwanadamu.
Wadau mbali mbali katika sekta ya elimu wanapaswa kutekeleza dhamana na wajibu huu
kwa ari na moyo mkuu, kwa kutambua kwamba, wamekabidhiwa amana na utajiri mkubwa kwa
ustawi na maendeleo ya sasa na kwa siku za usoni.
Mafanikio, matatizo na changamoto
zipembuliwe kwa uadilifu mkubwa, ili kupata matokeo yanayokusudiwa katika mchakato
wa kuleta maboresho katika mfumo wa elimu, ili kweli mwanadamu aweze kufikiri vyema
na kutenda kile anachofikiri kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi. Haya ni mambo
msingi katika mchakato wa maboresho ya elimu, ili kweli elimu iweze kuwa na manufaa
kwa vijana wa kizazi kipya, tayari kujikita katika ujenzi wa utamaduni wa haki, amani
na mshikamano.
Hii ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu
Francisko katika mazungumzo na wanafunzi wenye ulemavu kutoka sehemu mbali mbali za
dunia kama tukio la kufunga mkutano mkuu wa nne wa mitandao ya shule za kimataifa,
unaojulikana kama "Scholas Occurrentes" ulioanzishwa na Kardinali Jorge Mario Bergoglio,
wakati huo akiwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires, nchini Argentina, leo hii
mtandao huu unajumla ya shule 4000, zilizoenea sehemu mbali mbali za dunia. Mtandao
huu unawajumuisha wanafunzi katika masuala ya michezo, sayansi na teknolojia. Mkutano
huu ulikuwa unafanyika mjini Roma.
Baba Mtakatifu anasema, kila mwanafunzi
ni hazina muhimu sana inayopaswa kulindwa, kuheshimiwa na kuendelezwa. Vijana hao
kwa njia ya video wamesilimua shida, matatizo na changamoto wanazokutana nazo katika
maisha yao ya kila siku. Lakini bado wameweza kuvuka magumu yote haya kwa njia ya
matumizi sahihi ya teknolojia ya mawasiliano ya jamii pasi na kukata tamaa.
Mchakato
wa mageuzi ya elimu unaweza kusonga mbele kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika kukuza
na kudumisha mila na tamaduni njema za kijamii; kwa kuendeleza michezo, ili kuibua
karama na vipaji mbali mbali miongoni mwa vijana, tayari kusaidia maboresho ya maisha
ya vijana bila kusahau umuhimu wa kuwajengea vijana maarifa na ujuzi katika masuala
ya sayansi; mambo ambayo yanaweza kuwa ni madaraja ya kuwaunganisha watu katika jamii.
Vijana wajifunze kuheshimu na kuthamini mila na tamaduni zao njema, wasiwe
ni watu wa kuiga na kuchukua kila jambo kwani wanaweza kugenishwa hata katika tamaduni
zao wenyewe! Vijana pia wajitahidi kutafuta hekima ya Kimungu inayojikita katika Maandiko
Matakatifu; katika sanaa na uzuri, ili kukoleza kipaji cha ugunduzi kwa ajili ya mafao
ya wengi.
Baba Mtakatifu anawaalika wanafunzi kuonesha utajiri unaofumbatwa
katika maisha yao, ili kuwashirikisha na kuwamegea wengine, ili hazina hii iweze kuzaa
matunda na kuongezeka zaidi.Wajitahidi kujenga na kudumisha amani na utulivu ndani
mwao, kwa kuonesha uvumilivu, kwa kukubali mapungufu sanjari na kuheshimu tofauti.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.