2015-02-07 09:13:27

Baa la njaa na madhara yake!


Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, Jumapili tarehe 8 Februari, 2015 linaadhimisha Siku ya Mshikamano Kitaifa, ili kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Shirika la Misaada la Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, "Manos Unidas" katika mapambano dhidi ya baa la umaskini duniani, janga ambalo linaendelea kunyanyasa na kudhalilisha mamillioni ya watu sehemu mbali mbali za dunia.

Maadhimisho haya yanaongozwa na kauli mbiu" Mapambano dhidi ya baa la umaskini". Maaskofu wanawahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujinyima kidogo, kwa ajili ya kusaidia kasi ya mchakato wa mapambano dhidi ya baa la umaskini duniani, sanjari na ongezeko la njaa na utapiamlo, kashfa ya karne ya ishirini na moja!

Maaskofu wanasema, kuna kundi kubwa la watoto wanaoteseka na kufariki dunia wakiwa na umri mdogo kutokana na utapiamlo wa kutisha. Hili ni jambo la kusikitisha kwani kuna sehemu za dunia watu wanakula na kusaza, kiasi hata cha kujaza mapipa ya taka kwa chakula ambacho, kingeweza kusaidia mapambano dhidi ya utapiamlo wa kutisha, hapa kinachojitokeza ni utamaduni wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya wengine kama anavyobainisha Baba Mtakatifu Francisko.

Watu wakijiondoa katika ubinafsi, wakaanza ujenzi wa mshikamano wa udugu na upendo, kwa kuongozwa na dhamiri safi na nyofu; umaskini na njaa ni mambo yanayoweza kupewa kisogo na Jumuiya ya Kimataifa. Hapa kuna haja ya kubadili sera na mifumo ya kisiasa na kiuchumi, ili kupambana kufa na kupona na baa la njaa na umaskini wa hali na kipato! Umaskini si jambo la kudekezwa, kwani madhara yake ni makubwa katika maisha na maendeleo ya watu!

Maaskofu wanasema kwamba, ujenzi wa mshikamano wa upendo ni agizo la Kiinjili ambalo linapaswa kuvaliwa njuga na Familia ya Mungu, kwani watahukumiwa kadiri walivyowatendea ndugu zao katika shida na mahangaiko yao ya ndani. Kumbe, hapa kuna umuhimu wa kuelimisha na kukuza dhamiri nyofu, ili kusaidia mchakato wa maboresho unaopania kuifanya dunia kuwa kweli ni mahali pazuri zaidi pa kuishi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.