2015-02-06 08:28:15

Ni uhalifu dhidi ya binadamu!


Mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu ni changamoto inayoitaka Jamii kuhakikisha kwamba, inajifunga kibwebwe kungo'a mambo yote yanayopelekea ubaguzi na utengano katika jamii. Ni ujumbe kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Canada katika maadhimisho ya Siku ya kwanza ya kupambana na biashara haramu ya binadamu itakayoadhimishwa, Jumapili tarehe 8 Februari 2015 sanjari na kumbu kumbu ya Mtakatifu Josefina Bakhita, Mtawa wa Shirika ya Wakanosaa, aliyekombolewa kutoka utumwani na hatimaye, akaongoka na kuwa Mtawa, akajisadaka kwa ajili ya kuwahudumia watu waliokuwa wamekumbwa na athari za vita nchini Italia.

Hili ni tukio ambalo limeandaliwa na Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, Baraza la Kipapa la haki na amani pamoja na Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume Duniani. Changamoto kubwa kwa sasa ni kung'oa umaskini na ubaguzi; mambo yanayopelekea kushamiri kwa biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo. Hii ni changamoto ya kuhakikisha kwamba, sera na mikakati ya uchumi na maendeleo inatoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linabainisha kwamba, bado kuna umati mkubwa wa watu wanaoteseka na kuelemewa na umaskini wa hali na kipato; kuna sera za ubaguzi wa rangi na nyanyaso za kijinsia; licha ya harakati za jumuiya ya kimataifa kuhakikisha kwamba, watoto wanapata fursa ya kwenda shule, lakini bado kuna mamillioni ya watoto ambao hawana nafasi ya kuendelea na masomo na matokeo yake wanajikuta wanatumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu, utumwa mamboleo na kazi za suluba. Kuna magonjwa yanayotokana na afya ya akili; matumizi haramu ya dawa za kulevya; mambo ambayo kimsingi yanachagia kwa baadhi ya watu kutengwa na jamii.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linasema kwamba, hapa kuna haja ya kuwa na sheria na kanuni zinazotekelezeka katika medani mbali mbali za maisha ya binadamu, kwa kuwafikisha wahusika kwenye mkondo wa sheria na wahanga kusaidia tena kuanza ukurasa mpya katika maisha. Kuna umuhimu kwa Jamii kubadilishana mawazo, habari na takwimu, ili kujionea wenywewe athari na madhara ya biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linaungana na Baba Mtakatifu Francisko kuwapongeza na kuwashukuru watawa wa Mashirika mbali mbali wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya kuwalinda, kuwatetea na kuwahudumia wahanga wa biashara haramu ya binadamu na kwamba, hata wanasiasa na watunga sheria wanapaswa kutekeleza dhamana na wajibu wao, ili kutokomeza kabisa biashara haramu ya binadamu ambayo kimsingi ni uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.