Baba Mtakatifu Francisko ameyaandikia barua Mabaraza ya Maaskofu Katoliki pamoja na
Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kuonya kwamba, hakuna nafasi tena kwa
viongozi wa Kanisa watakaobainika wanajihusisha na vitendo vya unyanyasi wa kijinsia
dhidi ya watoto wadogo.
Barua hii ni mwendelezo wa juhudi za Kanisa kupambana
na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa kuunda Tume ya Kipapa kwa ajili ya kutetea
watoto wadogo, tume ambayo kwa mara ya kwanza tarehe 6 Februari 2015 imeanza kukutana
mjini Vatican. Tume hii iliundwa na Baba Mtakatifu Francisko, mwezi Machi 2014, kwa
lengo la kusaidia kutoa ushauri, mapendekezo, kanuni na sheria zitakazosaidia kuwalinda
watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia.
Ili kuiwezesha Tume hii ya Kipapa
kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara, Baba Mtakatifu amewateuwa watalaam na
wakereketwa wa nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo. Baba Mtakatifu katika
barua yake kwa viongozi wakuu wa Kanisa anawataka kusimama kidete, ili kuhakihakisha
kwamba, madonda ya nyanyaso za kijinsia ndani ya Kanisa yanakomeshwa na hatimaye,
kuanza mchakato wa upatanisho na uponyaji kwa wale wote waliofikwa na mkasa huu.
Hii
ni Tume ambayo ina wawakilishi kutoka sehemu mbali mbali za dunia na kwamba, Baba
Mtakatifu mwenyewe anasema, ameshuhudia machungu ya moyo kwa watu waliofikwa na mkasa
wa kunyanyaswa kijinsia, lakini pia ni watu ambao wana imani thabiti, licha madonda
ya ndani yanayowaandama.
Baba Mtakatifu anapenda kukumbusha kwamba, Kanisa
litaendelea kubainisha mbinu na mikakati ya kupambana na nyanyaso za kijinsia dhidi
ya watoto wadogo ndiyo maana, Tume hii ya Kipapa inatarajiwa kuwa ni chombo madhubuti
kwa Kanisa katika mchakato wa kupambana na nyanyaso za kijinsi dhidi ya watoto wadogo,
kwa kuhakikisha kwamba, Kanisa linatoa haki na kuonesha huruma kwa wale wote wanaofikwa
na mkasa huu.
Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuzihakikishia familia kwamba,
Kanisa linapenda kulinda na kuwapatia watoto mazingira bora zaidi ya makuzi na kwamba,
wasisite kuliendea kwa imani na matumaini. Hakuna nafasi tena ya "viongozi wa Kanisa
kulindana" ili kuepuka kashfa ya nyanyaso za kijinsia, kwani viongozi wanaojihusisha
na vitendo hivi vichafu hawana tena nafasi katika maisha na utume wa Kanisa.
Hapa
kuna haja ya kuhakikisha kwamba, sheria, kanuni na maadili vinafuatwa kwa umakini
mkubwa, kwa njia ya utekelezaji wa barua ya wazi iliyotolewa na Baraza la Kipapa la
Mafundisho Tanzu ya Kanisa kunako mwaka 2011. Ni wajibu wa Mabaraza ya JMaaskofu Katoliki,
kuandaa mbinu na mikakati ili kukabiliana na kashfa za nyanyaso za kijinsia.
Ni
vyema ikiwa kama Mabaraza ya Maaskofu Katoliki yataanzisha chombo cha kuratibu na
kufuatilia sheria na kanuni zilizobainishwa. Ni wajibu wa Maaskofu pamoja na Wakuu
wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kuhakikisha kwamba, yanaunda mazingira salama
kwa watoto na watu wazima wanaoweza kutumbukizwa kwenye kishawishi cha nyanyaso za
kijinsia.
Baba Mtakatifu anawaalika viongozi wa Kanisa kuhakikisha kwamba,
wanajiwekea utaratibu wa kuwahudumia wahanga wa nyanyaso za kijinsia: kisaikolojia
na katika maisha ya kiroho; viongozi wawe pia na ujasiri wa kukutana na wahanga pamoja
na familia zao. Huu ni muda muafaka wa kusikiliza na kuomba msamaha kwa wale waliotumbukizwa
katika kashfa hizi.
Baba Mtakatifu anayaalika Mabaraza ya Maaskofu katoliki
pamoja na Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kuhakikisha kwamba, yanashirikiana
kwa dhati na Tume ya Kipapa ya kutetea watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia.
Tume hii ni msaada mkubwa kwa viongozi wa Kanisa, kwa kubadilishana habari sanjari
na kuendeleza mchakato wa elimu, majiundo na uhamasishaji unaoweza kutoa majibu muafaka
dhidi ya nyanyaso za kijinsia.
Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha barua
yake kwa Maaskofu na Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kwa kumwomba Bikira
Maria, Mama mpole na mwingi wa huruma, alisaidie Kanisa kutekeleza wajibu huu kwa
ukarimu, kwa kutambua dhamana yake, tayari kulipia gharama za ukosefu wa haki kwa
kashfa zilizojitokeza huko nyuma, daima Kanisa liendelee kuwa aminifu, kwa kuwalinda
wale ambao Yesu mwenyewe alipenda kuwapatia kipaumbele cha kwanza.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.