Tanzania imesema kuwa dhamira yake ya kufungua balozi katika baadhi ya nchi duniani
iko pale pale na itatekeleza mpango wake huo kwa kadri hali ya fedha na uchumi inavyoruhusu.
Aidha, Tanzania imesema kuwa itaendelea kushirikiana na Iran katika kupambana na kukabiliana
na ugaidi duniani kwa sababu nchi mbili hizo, kama ilivyo dunia nzima, zinahitaji
dunia tulivu na inayosaka maendeleo ya watu bila usumbufu na matishio ya ugaidi.
Mambo
hayo mawili yamejadiliwa Jumatano, Februari 4, 2015 katika mazungumzo kati ya Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na Waziri wa
Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislam ya Iran, Mheshimiwa Javad Zarif.
Mheshimiwa
Zarif amewasili nchini Tanzania, Jumatano, akitokea Burundi katika ziara ambayo pia
imemfikisha Kenya, Uganda na Rwanda akifuatana na maofisa wa Serikali na kundi kubwa
la wafanyabiashara wa Iran. Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam,
Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Zarif kuwa Tanzania bado inakusudia kufungua ubalozi
mjini Teheran, mji mkuu wa Iran, kama ilivyoahidi na kuwa itafanya hivyo hali ya kifedha
na kiuchumi itakaporuhusu. Rais ametoa maelezo hayo kufuatia ombi la Waziri Zarif
kukumbushia umuhimu wa kuwepo kwa ubalozi wa Tanzania katika Iran.
“Tunakusudia
kufungua balozi katika nchi marafiki ambako kwa sasa hakuna balozi ikiwamo Jamhuri
ya Kiislam ya Iran. Katika Afrika, kwa mfano, tunapanga kufungua balozi katika nchi
ya: Namibia, Angola, Algeria na Ghana. Hizi ni nchi rafiki ambazo baadhi yake zimekuwa
na balozi katika Tanzania tokea uhuru wetu. Mbali na Iran katika Asia, tunaangalia
nchi kama Uturuki, Qatar na Kuwait na nchi nyingine marafiki,” Rais Kikwete amemwambia
Mheshimiwa Zarif.
Kuhusu mapambano dhidi ya magaidi, Rais Kikwete amesema kuwa
ni muhimu kwa Tanzania na Iran kuwa na msimamo ulio sawa wa jinsi ya kukabiliana na
ugaidi. “Wakati wote, sote tunakabiliwa na matishio ya ugaidi na hivyo tunalazimika
wakati wote kuwa macho na uwezekano wa mashambulizi ya kigaidi. Sisi Tanzania bado
tunakumbuka shambulio dhidi ya Ubalozi wa Marekani hapa nchini. Ulishambuliwa Ubalozi
wa Marekani lakini watu wote waliopoteza maisha yao ni Watanzania.”
Rais Kikwete
na Mheshimiwa Zarif pia wamejadili jinsi gani Tanzania na Iran zinavyoweza kuongeza
ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji katika maeneo mbali mbali ya uchumi na Rais
Kikwete amemweleza Waziri fursa zilizoko katika sekta za nishati na reli. Waziri Zarif
pia amemkumbusha Rais Kikwete mwaliko wa kumwomba Rais Kikwete kutembelea Iran kwa
ziara ya Kiserikali.