2015-02-04 10:11:26

Upatanisho na ujenzi wa taifa!


Askofu mkuu Telesphore Mpundu, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia anamwomba Rais Egdar Lungu na Serikali yake kujikita katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa na ujenzi wa Zambia kwani sasa pilika pilika za kampeni na hatimaye uchaguzi zimekamilika na uongozi unapaswa kuanza kutekeleza dhamana na majukumu yake barabara.

Katika mchakato wa upigaji kura, kila mtu alikuwa na mawazo na kiongozi wake aliyependa kumpatia kura yake kama sehemu ya utekelezaji wa Katiba na wajibu wa kiraia, kumbe, katika hili, taifa na wananchi wake walikuwa wamegawanyika, sasa ni wakati wa kuanza mchakato wa uponyaji unaojikita katika moyo wa msamaha na upatanisho, ili kukoleza utamaduni wa amani na utulvu.

Licha ya mchakato wa uchaguzi mdogo kumalizika kwa amani na utulivu, lakini kuna kasoro ndogo ndogo ambazo hazina budi kufanyiwa kazi kwa siku za usoni, ili kuhakikisha kwamba, Katiba ya nchi inalindwa na kuheshimiwa na wanasiasa wote. Kuwepo na amani na utulivu katika vyama vya kisiasa kabla ya kuanza kujikita katika kutafuta kura za wananchi ili kuongoza Taifa, kama ilivyojitokeza kwa vyama vingi vya kisiasa nchini Zambia.

Askofu mkuu Telesphore Mpundu anawataka wanasiasa kuhakikisha kwamba, wanatekeleza ahadi walizotoa kwa wananchi wakati wa kampeni, ili kuwajengea tena watu matumaini katika ushiriki wao kwenye masuala ya demokrasia na utawala bora. Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia linasikitika kusema kwamba, kuna baadhi ya wanasiasa wanatumia vyombo vya mawasiliano ya kijamii ili kupandikiza ukabila badala ya ujenzi wa umoja na mshikamano wa kitaifa; ukabila kwa sasa hauna mguso wala mashiko kwa watu.

Kanuni maadili za uchaguzi zinapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na wote na kwamba, viongozi wa Kanisa hawana sababu ya kujiingiza katika kampeni za uchaguzi kwa kuonesha upendeleo, changamoto ya kuangalia mapungufu yaliyojitokeza ili kujipanga vyema zaidi kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika tena nchini Zambia, kunako mwaka 2016. Tume huru ya uchaguzi Zambia haina budi kujengewa uwezo ili kuboresha Daftari la Wapiga kura pamoja na vituo vya kupigia kura.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.