Mediterrania: Mahali pa watu na tamaduni kukutana!
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, katika ujumbe wake kwa kikao cha
tisa cha wabunge kutoka katika nchi za Mediterrania, kilichoanza Jumatatu tarehe 2
Februari na kuhitimishwa tarehe 4 Februari 2015, anakumbusha kwamba, Mediterrania
inapaswa kuwa ni mahali pa watu kukutana na kamwe isitumike kwa ajili ya vita, kinzani
na chuki kwa kisingizio cha kidini.
Wajumbe wanapaswa kutoa majibu muafaka
ili kukabiliana na changamoto ya wahamiaji na wakimbizi wanaotafuta usalama na ubora
wa maisha Barani Ulaya; makundi ambayo kwa bahati mbaya yanatumbukia mikononi mwa
watu ambao dhamiri zao zimekufa na matokeo yake, ni kuwasukumiza katika biashara haramu
ya binadamu na utumwa mamboleo.
Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko anasema
Kardinali Parolin kwamba, wajumbe wataweza kuibua mbinu mkakati utakaosaidia ujenzi
wa mchakato wa watu kukutana katika Ukanda wa Mediterrania. Kwa sasa nchini hizi zinakabiliwa
na changamoto nyingi kutokana na kinzani za kisiasa kutoka katika baadhi ya nchi za
Kiafrika, vita na vitendo vya kigaidi huko Syria na Iraq.
Inasikitisha kuona
kwamba, katika kipindi cha mwaka 2014 vitendo vya kigaidi vimeongezeka maradufu kiasi
cha kutishia usalama, amani na haki msingi za binadamu. Vatican kwa upande wake inahofia
usalama na maisha ya Wakristo huko Mashariki ya Kati pamoja na kutambua kwamba, kuna
Waislam ambao pia wanateseka na kunyanyasika kutoka kwa waamini wenye misimamo mikali
ya kiimani.
Lakini ikumbukwe kwamba, kamwe, vita kwa kutumia jina la Mungu
haviwezi kuhalalishwa kama anavyokemea Baba Mtakatifu Francisko. Vitendo hivi havina
budi kukemewa na kulaaniwa kwa "macho makavu bila kusita" hata na viongozi wa dini
ya Kiislam. Kwa miaka mingi Mediterrania imekuwa ni eneo la makutano kati ya watu
na tamaduni mbali mbali, changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, eneo hili
linaendelea kuwa ni uwanja wa watu na tamaduni kukutana, kwa amani na utulivu.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.