Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr. Jakaya Mrisho Kikwete amemteua Dkt. Hamisi
Hassan Mwinyimvua kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, anayesimamia Menejimenti
ya Fedha za Umma (Public Finance Management). Kabla ya uteuzi wake, Dkt. Mwinyimvua
alikuwa Msaidizi wa Rais wa muda mrefu wa masuala ya uchumi.
Taarifa iliyotolewa
na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Yohana Sefue Jumatatu, Februari 2,
2015, imesema kuwa uteuzi wa Dkt. Mwinyimvua ulianza Jumamosi, Januari 24, 2015. Dkt.
Hamisi Hassan Mwinyimvua ni mwanataaluma mwenye ujuzi na uzoefu mkubwa katika masuala
ya uchumi.
Anayo shahada ya kwanza ya B.A. (Econ) ya Uchumi kutoka Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam (1986), Shahada ya Uzamili ya M.A. (Econ) ya Uchumi kutoka Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam (1988) na Shahada ya Uzamivu ya uchumi kutoka vyuo vikuu vya
Dar es Salaam na Lund cha Sweden.
Dkt. Mwinyimvua amekuwa mhadhiri wa miaka
mingi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambako amepanda daraja kutoka “Tutorial
Assistant”, mwaka 1986-1988, Mhadhiri Msaidizi, mwaka 1988-1996, Mhadhiri, mwaka 1996-2005,
Mhadhiri Mwandamizi, mwaka 2005-2006 na Mkuu wa Idara ya Uchumi ya chuo hicho mwaka
2006. Dkt. Mwinyimvua aliteuliwa kuwa Msaidizi wa Rais, Uchumi, mwaka 2006, nafasi
ambayo ameishikilia hadi mwaka huu, 2015.