2015-02-03 10:44:39

Si haba! Yataka moyo!


Mama Kanisa anaendelea kuadhimisha Mwaka wa Watawa Duniani, kwa kuwahimiza watawa kuwa kweli ni mashuhuda wa Furaha ya Injili na Manabii wanaowatangazia Watu wa Mataifa matendo makuu ya Mungu kwa njia ya huduma makini mintarafu karama za Mashirika ya kitawa na kazi za kitume.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka watawa kuyapyaisha maisha na utume wao kwa kuonesha utii na uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, tayari kujisadaka kwa ajili ya kuwaamsha walimwengu, kwa njia ya Uinjilishaji mpya.

Kardinali Joao Braz de Aviz, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na kazi za kitume anasema, Baba Mtakatifu anapenda kuwashirikisha watawa ile furaha ya kweli inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, licha ya magumu na changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume wao, hususan katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Maisha ya kitawa na kazi za kitume ni sehemu ya mchakato wa mwendelezo wa majadiliano ya kiekumene, ili kuwawezesha Wakristo wa Makanisa na Madhehebu mbali mbali kumshuhudia Kristo, kwa njia ya sala, huduma na majadiliano ya kina, cheche ambazo Kardinali Joao Braz di Aviz anasema, zimejionesha kwa mara ya kwanza wakati wa maadhimisho ya Juma la kuombea umoja wa Wakristo sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Watawa.

Hii ni changamoto kubwa kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko anayewahamasisha waamini kujenga madaraja na utamaduni wa kukutana, kupendana na kusaidiana, ili kuweza kushirikishana uzoefu na mang'amuzi ya uwepo wa Mungu kati yao! Makanisa ya Mashariki na Watawa wao, wana utajiri mkubwa katika maisha ya kiroho; mambo ambayo watawa wanaweza kushirikishana kama sehemu ya mchakato wa kutajirishana, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Majadiliano ya kiekumene yanayofumbatwa katika maisha ya kitawa na kazi za kitume, yalenge kukoleza moyo wa kufuasa Kristo zaidi, ili kumshuhudia kati ya Watu wa Mataifa; kwa kuendelea kujikita katika toba na wongofu wa ndani, sanjari na kusoma alama za nyakati.

Kuna umati mkubwa wa watawa wanaojisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, lakini kwa masikitiko makubwa, Baba Mtakatifu anashangaa kuona jinsi ambavyo kila mwaka kuna watawa wa kike na kiume wanaoamua "kubwaga manyanga" na kuanza maisha mapya. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna watawa zaidi ya millioni moja na nusu wanaoishi na kufanya kazi na utume wao katika Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume elfu tatu!

Kumbe, inasikitisha kuona watawa wakiacha wito wao na kuamua kufuata njia nyingine ya maisha! Hapa kuna haja ya kufanya tafakari ya kina, ili kuboresha hali ya maisha inayowatatiza watawa, ili hatimaye, waweze kujisikia kweli wako nyumbani na kuendelea kudumu hadi pale Mwenyezi Mungu atakapowaita kutoka katika dunia hii!.

Baba Mtakatifu anawaalika watawa kuangalia mambo makuu matatu: mang'amuzi ya maisha na wito wa kitawa, jambo ambalo linapaswa kufanywa kwa uangalifu mkubwa kwa kutambua lengo kuu linalomsukuma kijana kuacha yote kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake! Pale maamuzi na malengo yanaposigana, si haba kuona kwamba, watu wanaamua kuacha wito na maisha ya kitawa.

Hatua ya pili muhimu ni majiundo makini ya awali na endelevu; hapa ikumbukwe kwamba, watawa wanafundwa si tu na mtu mmoja ambaye ameteuliwa kuwa ni mlezi, bali jumuiya na mahali ambapo malezi haya yanafanyika bila kusahau athari za jamii inayowazunguka. Watawa wanapaswa kutambua kwamba, daima wao ni sehemu ya mchakato wa majiundo endelevu, hadi pale watakapoingia kaburini.

Majiundo makini yalenge kuwasaidia watawa kumfuasa Kristo: fukara, mseja na mtii, kwa kujikita katika karama za waanzilishi wa Mashirika yao, tayari kusoma alama za nyakati ili kuzipyaisha na kuzimwilisha katika uhalisia wa watu wanaowahudumia kwa sasa.

Baba Mtakatifu anasema, hatua ya tatu ni ile inayopasa kumwangalia mtawa kama sehemu ya fumbo la maisha ya mwanadamu; mwanadamu ataendelea kubaki kuwa ni fumbo kwake mwenyewe na hata kwa wale watu wanaomzunguka, ndiyo maana kuna haja ya kujenga na kudumisha utamaduni wa kusikilizana katika ukweli na uwazi, ili kulifahamu fumbo la maisha ya mwanadamu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.