2015-02-03 12:16:58

Rais wa Italia!


Bwana Sergio Mattarella, baada ya kula kiapo cha utii kwa Katiba ya Nchi, kuhutubia Bunge na Taifa kwa ujumla, akapigiwa mizinga ishirini na moja pamoja na kutembelea Altare ya wahenga wa Italia, kuanzia tarehe 3 Februari 2015 anakuwa ni Rais wa kumi na mbili wa Italia.

Katika hotuba yeke ya kwanza kama Rais wa Italia, amekazia kwa namna ya pekee umoja na mshikamano wa kitaifa ili kupambana na ukosefu wa haki, umaskini na upweke ili kuanza mchakato wa kuwajengea wananchi wa Italia matumaini mapya, kwa kuwapatia haki na huduma msingi za kijamii. Kuna kundi kubwa la vijana wasiokuwa na fursa za ajira, hawa wanapaswa kusaidiwa, ili kuwa na matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi kwa kufanya maboresho makubwa katika sekta ya uchumi.

Rais Mattarella anawataka wafanyakazi wa Serikali kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia misingi ya ukweli, uwazi, uadilifu na uwajibikaji; makini katika maneno na matendo yao. Ametaka wanasiasa kufanya mabadiliko ya kweli katika uwanja wa kisiasa, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya taifa na kwamba, uongozi ni huduma sanjari na kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya Katiba ili kuimarisha demokrasia. Kama Rais atasimamia, kulinda na kutetea Katiba ya Nchi.

Rais Mattarella anamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa ujumbe wa matashi mema aliyomwandikia hivi karibuni, anaungana naye kulaani rushwa na ufisadi wa mali ya umma; ukosefu wa haki, amani na utulivu na kwamba, kwa sasa vitendo vya kigaidi vinatishia usalama na mfungamano wa kijamii katika ngazi mbali mbali. Hapa kuna haja ya kuachana na tabia ya chuki na kupenda kulipizana kisasi; mambo ambayo yameigharimu Italia kwa kiasi kikubwa.

Rais Mattarella anaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuvalia njuga tatizo la vitendo vya kigaidi, ili kuwahakikishia watu usalama wa maisha na mali zao; amani na matumaini. Anasema vita kwa malengo yoyote yale, haina tena mashiko wala mvuto bali itaendelea kusababisha majanga, kumbe kuna haja ya kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na maridhiano kati ya watu.

Italia itaendelea kushirikiana kwa hali na mali katika mahusiano ya kimataifa na kwa namna ya pekee kabisa amemkumbuka Padre Paolo Dall'Oglio na wengine ambao wametekwa nyara na hadi sasa hawajulikani mahali walipo. Watu wanataka kuwa huru, kwa kuishi katika amani na mshikamano; watu wanaojisiia kuwa kweli ni Jumuiya inayojikita katika mchakato wa ujenzi wa matumaini mapya.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.