Jumatatu asubuhi Papa Francisko alikutana na kikundi cha Maaskofu kutoka Lithuania
ambyo wako katika ziara yao ya kitume katika Kiti Kitakatifu na idara za Curia ya
Roma kwa ujumla.
Papa Francisko aliwapokea kwa moyo mkunjufu wa kibaba huku
akionyesha kutambua ushupavu wao, hasa kwa maaskofu waliopita katika kipindi kigumu
cha mateso ya wakati wa kipindi cha ukomunisti nchini mwao. Amewashukuru kwa kudumu
kuwa mashahidi wa Yesu Kristo na huduma yao kwa watu wa Mungu.
Papa aliendelea
kuonyesha kutambua changamoto zinazo wakabili katika kazi zao za kitume. Na kwa jinsi
Kanisa kwa muda mrefu katika nchi yao, limepambana na madhulumu kutoka serikali iliyojengwa
katika misingi ya itikadi zilizo kinyume na hadhi na uhuru wa binadamu. Licha ya hilo
pia sasa wanakabiliwa na hatari nyingine, kama vile ukana Mungu na dharau kwa dini
kuwa ni mambo ya mpito wa nyakati. Kutokana na hali hizi , ni wazi utangazaji wa
Injili na maadili ya Kikristo, inakuwa ni jambo muhimu, bila kusahau mjadala wa kujenga
umoja na mshikamano na wote, hata kwa na wale wasio thamini Kanisa au wale waliojitenga
mbali na maisha ya kidini. Ni muhimu kuwa karibu na wote kama chumvi na mwanga na
kichocheo kwa jamii nzima katika harakati za kufanikisha manufaa ya wote.
Katika
changamoto hizo zote hizo, Papa amesema silaha kuu ya kupata ushindi ni kudumu katika
sala na maombi. Na pia kumwomba Mungu, awajalie Mapadre wakarimu walio yatoa maisha
yao kweli sadaka na kujituma. Na hata waamini wa kawaida, nao wawe na ufahamu wa kutosha
juu ya majukumu yao ndani ya jumuiya ya kanisa na umuhimu wa kutoa mchango wa Kikristo
katika jamii.
Na kama wanavyofahamu kwa kipindi hiki, Kanisa zima linashiriki
katika mchakato wa kutafakari juu ya familia, uzuri wake, thamani yake, na changamoto
ni zinazo wakabili katika wakati wetu. Hivyo wao kama wachungaji, wanapaswa kutoa
mchango wao kwa kazi hii kubwa ya utambuzi, na hasa kupata majawabu yanayofaa kwa
huduma za kichungaji kwa familia, ili wanandoa waweze kusikia kwa ukaribu zaidi
kuwa ni sehemu yajamii ya Kikristo na wasaidiwe kupambana na changamoto za dunia ya
kileo, daima wakijisikia wapya katika roho ya Injili "(Rum 12,2).
Papa pia
alipendekeza kipaumbele maalum kwa miito ya ukuhani na maisha wakfu, akiwaomba wasali
bila kuchoka kwa ajili ya miito. Na lazima watoe mafunzo ya kutosha, tangu mwanzo
wa malezi kwa ajili ya upadri, maisha wakfu, kwa waliojiunga na maisha hayo seminarini.
Ni lazima kutoa kipaumbele maalum kwa maisha yao ya kiroho na kimaadili, na elimu
na umaskini wa Kiinjili na usimamizi wa mali na nyenzo kulingana kanuni za mafundisho
ya kijamii ya Kanisa.
Mwisho Papa aliwasihi wasisahau huduma kwa maskini.
Watu wasiokuwa na ajira, wagonjwa na walio telekezwa. Na pia vijana, wanaotaka kuondoka
kwa sababu mbalimbali kwenda kutafuta njia mpya za maisha je ya nchi. Wote wanahitaji
huduma za kichungaji kutoka Baraza la Maaskofu, ili waweze kudumu katika imani yao
na taratibu za kidini za Lithuania.