Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameutaka uongozi wa Bodi ya Mamlaka ya Vyuo
Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) nchini uelekeze jicho lake Nyanda za Juu Kusini
na kuandaa vijana wenye weledi na stadi ya uchimbaji madini ili kukabili changamoto
za soko.
Ametoa wito huo Jumamosi, Januari 31, 2015 wakati akizungumza na
walimu na wanafunzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) cha Songea mjini, mkoani
Ruvuma ambako pia alikabidhi vyerehani 20 vyenye thamani ya sh. milioni 4/- kwa wanafunzi
20 waliohitimu kozi ya ushonaji mwaka 2014.
Waziri Mkuu ambaye aliwasili
Songea mjini Ijumaa jioni akitokea Dodoma, alifanya kazi hiyo ya kukabidhi vyerehani
ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa Julai 20, 2013 wakati akizindua chuo hicho
alipofanya ziara ya kikazi kwenye mkoa huo. “Katika kipindi kifupi, mkoa wa Ruvuma
umeanza kubadilika kwa kasi ya haraka. Kuna madini ya urani, makaa ya mawe na dhahabu.
VETA inapaswa iangalie fursa hii kwa kuandaa vijana wenye stadi za uchimbaji madini
ili wakati wawekezaji wakianza kuchimba tayari muwe na watu wa kufanya hiyo kazi kutoka
kwenye mkoa huu,” alisema Waziri Mkuu.
“Wasilianeni na Wizara ya Nishati
na Madini ili mjue mahitaji yao kwenye eneo hili ni yapi. Wakianza uchimbaji watataka
watu wa kufanya kazi hizo. Andaeni vijana... siyo mkae tu na kuja kushtukizwa au mjikute
vijana kutoka mbali wanapata hizo ajira wakati wa kwenu wangeweza kunufaika na fursa
hii,” alisema.
Aliwataka vijana wanaosoma katika chuo hicho wasome kwa
bidii na kuacha kasumba ya kuchagua kazi na kuonea aibu baadhi ya kazi. “Someni, someni
sana kwa sababu ustawi wa maisha ya Mtanzania hapo baadaye unategemea elimu ya ufundi.
Tuachane na fikra potofu za kuchagua kazi. Kama ni mpishi fanya kazi ya upishi vizuri
sababu walaji wapo, hawaishi,” alisisitiza.
Alisema VETA inaweza kuwa suluhisho
la ukosefu wa ajira hapa nchini kwa sababu ufundi na stadi wanazopata wahitimu wa
vyuo hivi vinapaswa kuwapatia ajira. “Tanzania ina wakazi milioni 45 na wote hawa
wanataka kuvaa. Mkianzisha kikundi kidogo kuamua kushona tu sare za shule, tayari
mtakuwa mmetoa jibu kwa hitaji la sare za wanafunzi. Wamachinga watanunua kwenu na
kuuza lakini na ninyi pia mtapata fedha kuendeshea mradi wenu,” aliwasisitizia wahitimu
hao.
Mapema, akisoma risala ya chuo hicho, Mwenyekiti wa Bodi ya VETA Kanda
ya Nyanda za Juu, Bw. Kabaka Ndenda alisema chuo hicho kimekwishatoa wahitimu wa kozi
fupi 2,627 katika fani mbalimbali za mafunzo ambapo kati yao wavulana ni 2,202 na
wasichana ni 425. Aliiomba Serikali iiangalie VETA kisera zaidi kama mkombozi wa ajira
hasa wakati huu ambapo vijana wengi wanakabiliwa na ukosefu wa ajira. Alizitaja baadhi
ya kozi zinatoloewa chuoni kuwa ni mafunzo ya udereva wa magari na pikipiki; uhazili;
utengenezaji wa kompyuta; umeme wa jua; umeme wa majumbani; ulimbwende (cosmetology)
na upishi.
Alisema chuo hicho kwa sasa kina wanafunzi 298 wanaoendelea na
kozi mbalimbali na mwaka huu kinatarajia kudahili wanafunzi 306.