2015-02-02 14:40:00

SECAM yaanza mkutano Vatican


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, kuanzia tarehe 2 hadi tarehe 8 Februari 2015 limeanza mkutano wake mjini Vatican, utakaokuwa ni fursa ya kuzungumza na kujadiliana na viongozi mbali mbali wa Sekretarieti ya Vatican, kuhusu hali ya maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika. Viongozi wakuu wa SECAM watapata pia fursa ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mkutano wao hapa mjini Vatican.

Ujumbe wa viongozi wakuu wa SECAM unaongozwa na Askofu Gabriel Mbilinyi, Rais wa SECAM. SECAM itapitia tena mikakati ya ushirikiano na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, CCEE, hasa zaidi kuhusiana na semina itakayojadili tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, inayotarajiwa kufanyika nchini Msumbiji, mwezi Mei, 2015.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.