Mons. Liberatus Sangu ateuliwa na Baba Mtakatifu kuwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki
la Shinyanga, Tanzania!
Baba Mtakatifu Francisko amemteua Monsinyo Liberatus Sangu kutoka Jimbo Katoliki la
Sumbawanga, kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Shinyanga, Tanzania. Kabla ya uteuzi
wake, Askofu mteule Sangu alikuwa ni Afisa mwandamizi katika Baraza la Kipapa la Uinjilishaji
wa watu mjini Vatican.
Askofu mteule Liberatus Sangu alizaliwa kunako tarehe
19 Februari 1963, Kijijini Mwanzye, Jimbo Katoliki la Sumbawanga. Baada ya masomo
na majiundo yake ya kikasisi kwenye Seminari kuu la Kibosho, Jimbo Katoliki Moshi
na Segerea, Jimbo kuu la Dar es Salaam, akapadrishwa kunako tarehe 9 Julai 1994.
Katika
maisha yake kama Padre, Askofu mteule Sangu amewahi kuwa Mlezi wa Seminari ndogo ya
Kaengesa, Jimbo Katoliki la Sumbawanga kuanzia mwaka 1994 hadi mwaka 1995. Akateuliwa
kuwa Paroko wa Parokia ya Matai kuanzia mwaka 1995 hadi mwaka 1996. Kati ya Mwaka
1996 hadi mwaka 1999 alikuwa mjini Roma kwa masomo ya juu na kujipatia shahada ya
Uzamili katika taalimungu ya Sakramenti za Kanisa, kutoka katika Chuo Kikuu cha Kipapa
cha Mtakatifu Anselmi, kilichoko mjini Roma.
Kuanzia mwaka 1999 hadi mwaka
2000, aliteuliwa kuwa Msimamizi wa Parokia ya Mwanzye. Kuanzia mwaka 2000 hadi mwaka
2007 akateuliwa kuwa ni Mkurugenzi wa miito Jimbo Katoliki la Sumbawanga; mlezi katika
mwaka wa malezi na mkurugenzi wa utume wa vijana, Jimbo Katoliki Sumbawanga. Kunako
mwaka 2007 hadi mwaka 2008 aliteuliwa kuwa Paroko wa muda Parokiani Sopa. Kuanzia
mwaka 2008 hadi uteuzi wake, amekuwa akitekeleza utume wake kama Afisa mwandamizi,
Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu mjini Vatican.
Itakumbukwa kwamba,
Jimbo Katoliki la Shinyanga, Tanzania kuanzia mwaka 2012 limekuwa wazi kufuatia kifo
cha Askofu Aloysius Balina.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya
Kiswahili ya Radio Vatican.