2015-02-02 13:51:03

Amua!


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo. Tunanakukaribisha kwa mara nyingine tena tuendelee kukitegea sikio kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani. Kwa vipindi vilivyopita tulitazama familia kama shule ya maadili na fadhila mbalimbali. RealAudioMP3

Lengo letu: tunataka familia zetu na taasisi zote za malezi, ziwe vitalu vya kuandaa watu wema, watu wenye kufaa kulijenga taifa na Kanisa. Pasipo kuwekeza katika malezi bora kwa watoto wetu, hapo tujue kwamba tunachangia kwa kiasi kikubwa kuangamia kwa kizazi kijacho.

Tukichunguza kwa makini kabisa na kwa jicho-wajibifu, tutaona ishara mbalimbali zinajitokeza ambazo zinaashiria kwa uwazi kabisa uangamizi wa kizazi kijacho. Ishara hizo ni pamoja na watu kutokujipenda kwa kujiweka daima katika matendo hatarishi; wazazi kutopenda kuwa jirani na watoto wao, kwa kisingizio cha kazi na utafutaji wa mali, uadui usioelezeka unaojengeka kati ya watoto na wazazi, watu kuchukiana kwa viapo na kutopenda kabisa kusameheana, kukua kwa tabia ya kuchukia uhai, kuongezeka kwa roho mbaya, kukosa kabisa kuthamini utu na badala yake kujali zaidi mali na fedha.

Kuna ongezeko la tabia ya kutokutunza mazingira, kitu ambacho ni urithi wetu kwa kizazi kijacho; wenye dhamana ya kutoa elimu kwa watoto wetu, kutothamini uadilifu na ubora wa elimu, jambo ambalo linachangia kuandaa akili-tundu kwa watoto wetu. Mambo haya na mengine mengi yanayofanana na hayo ni ishara za mchango wetu kwa uangamizi wa kizazi kijacho.

Tufanye nini basi? Pamoja na kuiangazia familia kama shule ya maadili, sisi sote tulialikana na tunaendelea kualikana kujibidisha katika majiundo binafsi, yaani kukomesha kabisa vilema vyetu vya roho na mwili, kujikuza zaidi katika fadhila, ili sisi wenyewe tuwe watu tunaojifaa na kuwafaa jirani zetu. Katika maisha yetu ya kila siku kuna wakati huwa tunatambua mapungufu yetu iwe ni kwa kuambiwa au kwa kujua sisi wenyewe.

Lakini huwa inakuwa vigumu sana kujikubali na kujichukulia hatua! Tunajiogopa sisi wenyewe hadi tunashindwa kujipatia katazo binafsi, kujiwekea mkakati mpya wa kuinuka na kusonga mbele. Ndio maana tunabaki katika makosa yaleyale, vilema vilevile miaka yote. Tunajitesa na kutesa familia, jamaa na majirani kwa vilema vyetu ambavo kwa kiburi kikavu tu, na uzembe-baridi hatutaki kujikwamua na kujirekebisha. Jipe moyo, chukua hatua, unaweza kubadilika na kuwa mwema zaidi na zaidi. Amua sasa!!

Pamoja na majiundo binafsi, tusikose kuliinamishia sikio-zikivu Kanisa Takatifu. Tumsikilize kwa makini mama Kanisa mtakatifu ambaye daima anatupa miongozo ya utu wema. Dhamiri zetu ziwe na hofu ya Mungu. Hofu ya Mungu inatusaidia kutenda yote kwa roho ya uwajibikaji na kujali mafaa adilifu ya wengi. Pasipokuwa na hofu ya Mungu, daima tutatenda mambo hatarishi ambayo yatatuangamiza sisi wenyewe na hatimaye kuandaa mazingira na mifumo angamizi kwa kizazi kijacho. Neno hili litusaidie kujenga dhamiri-wajibifu kwa kizazi kijacho. Tutambue kwa dhati kwamba, hali yoyote, iwe njema au mbaya kwa kizazi kijacho hutegemea zaidi mifumo tunayoiweka sisi tunaoishi sasa.

Kwa kuzingatia ukweli huo ndio maana Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, akitufundisha juu ya dhambi saba za jamii, alitaja mambo kama uharibifu wa mazingira na maonezi ya kijamii. Kwa uharibifu wa mazingira tunakidhulimu kizazi kijacho haki ya kuishi katika mazingira bora. Kwa maonezi ya kijamii, tunaandaa watu wenye hasira, wasiojipenda, wenye chuki kali kwa wenzao, wenye roho ya kulipiza visasi, wasiojisikia vizuri kuishi duniani hapa.

Tunaahirisha kipindi chetu cha leo kwa kunidhamishana neno hili: kila mmoja wetu ajiunde hivi ili awe mtu wa kufaa katika jamii inayomzunguka. Nasi sote kwa pamoja tuone na tuonje kwa dhati kuwa ni wajibu wetu wa dhati kabisa kuandaa mazingira bora kwa kizazi kijacho. Kizazi kijacho tunacho tayari mikononi mwetu. Tujiulize daima, tunataka jamii yetu iwe ya aina gani?

Tusikilizani tena kipindi kijacho!! Kutoka katika studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB








All the contents on this site are copyrighted ©.