Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kichungaji Injili ya Furaha, Evangelii
gaudium, anaonesha msisitizo wa pekee katika mahubiri, changamoto ambayo ilikwishawahi
kutolewa na Mababa wa Sinodi na hatimaye, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI akakazia
zaidi katika Nyaraka zake za kitume, Neno la Mungu, Verbum Domini na
Sakramenti ya Upendo, Sacramentum caritatis.
Huu ni mwendelezo wa changamoto ambazo zilifanyiwa kazi na Mababa wa Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu umuhimu wa Liturujia katika maisha na utume wa Kanisa
na matokeo yake, Baraza la Kipapa la Ibada, Nidhamu na Sakramenti za Kanisa limetoa
Mwongozo kwa ajili ya mahubiri.
Mwongozo huu umegawanyika katika sehemu kuu
mbili: Sehemu ya kwanza inahusu mahubiri katika Liturujia. Hapa Baraza linafafanua
asili na umuhimu wa mahubiri sanjari na mambo msingio yanayoambatana na mahubiri,
yaani Mklero aliyewekwa wakfu kwa ajili ya kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa na mwenye
dhamana ya kusoma na kulifafanua Neno la Mungu. Ni kiongozi anayepaswa kujiandaa kikamilifu
kabla ya kuingia Altareni, ikiwa ni pamoja na kuwatambua waamini au wasikilizaji wake.
Sehemu ya pili ya Mwongozo huu inahusu sanaa ya kuhubiri, inayopembua kwa kina
na mapana mbinu na maudhui yanayopaswa kuwasilishwa mbele ya Familia ya Mungu wakati
wa mahubiri. Kuna mwongozo wa namna ya kuhubiri katika Jumapili za kawaida, wakati
wa Sherehe na Siku kuu, lakini kwa namna ya pekee wakati wa Kipindi cha Juma kuu,
Kwaresima, Majilio, Noeli na Kipindi cha Mwaka wa Kanisa. Kuna maelezo ya kina kuhusu
mahubiri wakati wa matukio maalum kwa maisha ya waamini, kwa mfano wakati wa kufunga
ndoa au mazishi.
Hapa kuna mambo msingi ambayo yanapaswa kugusiwa wakati wa
mahubiri kutoka katika Maandiko Matakatifu, Agano la Kale, Agano Jipya na Injili.
Hapa mkazo unawekwa kwenye Liturujia ya Neno la Mungu na Liturujia ya Ekaristi pamoja
na mpango mzima wa maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Hapa kuna ujumbe unaogusa
Biblia na Ekolojia katika maadhimisho ya fumbo la maisha; kati ya kusikiliza Neno
la Mungu pamoja na kuzingatia adhira inayokusudiwa.
Baraza la Kipapa la Ibada,
Nidhamu na Sakramenti za Kanisa, mwishoni, linaweka kiambatanisho kinachoonesha uhusiano
uliopo kati ya Mahubiri na Mafundisho ya Kanisa Katoliki kwa kuweka mkazo wa pekee
kwa wahubiri kufanya rejea katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Kiambatanisho
cha pili kinaonesha baadhi ya nyaraka za Mababa Watakatifu kuhusiana na mahubiri.
Muswada
wa mwongozo huu baada ya kufanyiwa tathmini ya kina na wajumbe wa Baraza la Kipapa
la Ibada, Nidhamu na Sakramenti za Kanisa na hatimaye kupitishwa wakati wa maadhimisho
ya mkutano mkuu wa Baraza uliofanyika Mwezi Februari na Mei, 2014, ukapelekwa kwa
Baba Mtakatifu Francisko ambaye ameagiza kwamba Mwongozo huu uchapwe kwa ajili ya
kuwasaidia Wakleri katika kutangaza Injili ya Furaha kwa njia ya mahubiri, yaliyoandaliwa
kwa umakini mkubwa, ili kuzima kiu ya udadisi wa kutaka kufahamu undani wa Maandiko
Matakatifu.
Ni matumaini ya Baraza kwamba, Mwongozo huu utasaidia waamini
kukutana kwa furaha na mwanga wa Roho Mtakatifu kwa njia ya mahubiri, kwa kujikita
katika Neno la Mungu na wala si kwa ajili ya kuwafurahisha walimwengu. Mwongozo huu
utafanyiwa tafsiri katika lugha mbali mbali, lakini kwa kuratibiwa na Baraza la Kipapa
la Ibada, Nidhamu na Sakramenti za Kanisa.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.