2015-01-29 08:36:40

Jeuri ya kujisadaka kwa ajili ya Kanisa!


Wakumbatieni watu kwa njia ya upendo wa Mungu, ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, CEI, katika maadhimisho ya Siku ya kumi na tisa ya Watawa Duniani, yanayofanyika kila mwaka ifikapo tarehe 2 Februari, sanjari na maadhimisho ya Siku kuu ya Kutolewa Bwana Hekaluni. Kwa mwaka huu, Siku ya Watawa Duniani, inaadhimishwa sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linawaambia Watawa kwamba, Familia ya Mungu inapenda kuwaona watawa wakishuhudia kwa maisha na utume wao, wokovu ambao umefunuliwa na Mwenyezi Mungu kwa Watu wa Mataifa kwa njia ya Yesu Kristo. Watawa wawe na ujasiri wa kusoma alama za nyakati, ili kuvuka vikwazo vinavyoweza kuwaandama na kukinzana na maisha pamoja na utume wao. Watembee katika mwanga angavu, huku wakitafuta amani na utulivu wa ndani. Hii ndiyo siri kubwa ya urembo, inayowatofautisha watu ambao wamejisadaka na kujiweka wakfu mbele ya Mungu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.

Watawa wawe na ujasiri wa kuangalia matukio mbali mbali ya maisha, kwa uwazi na uhuru kamili; kwa kupima na kuchambua mambo, bila kumtenga wala kumbagua mtu, kwani binadamu wote wanapaswa kukumbatiwa na upendo na huruma ya Mungu inayoshuhudiwa kwa njia ya ushuhuda wa maisha ya kinabii yanayotolewa na watawa.

Baba Mtakatifu Francisko katika barua yake kwa maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani anasema kwamba, watawa wanapaswa kuwa kweli ni chemchemi ya furaha kwa wale wanaowazunguka, kwa kutambua kwamba, wao katika maisha na utume wao, ni kielelezo makini cha Mwenyezi Mungu anayewaokoa watu wake. Katika maisha, watawa watakumbana na kinzani, mchoko na hata wakati mwingine kukata au kukatishwa tamaa.

Wamebarikiwa Watawa wanaosaidiana na kutaabikiana, ili wasije kuanguka na hatimaye, kumezwa na malimwengu. Waoneshe ari, moyo na ujasiri wa kutaka kuendelea kumfuasa Yesu Kristo aliyekuwa: mtii, mseja na fukara. Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linaweka matumaini yao makubwa kwa watawa, kwa mchango wao unaoweza kusaidia kuharakisha mchakato wa mageuzi katika maisha ya Kikristo kwa kuonesha njia mpya za kumwilisha Injili ya Kristo katika uhalisia wa maisha sanjari na kupambana na changamoto za maisha zinazojitokeza kwa sasa.

Baba Mtakatifu anawakumbusha watawa kwamba, anasubiri kuona makali yao, kwa kujenga mazingira yatakayosaidia kukuza na kudumisha moyo wa sadaka na majitoleo; kwa kukuza udugu na ukarimu hata katika tofauti zao, ili kuweza kushirikishana upendo unaokoa. Maisha na utume wao vishuhudie jinsi ambavyo wanajitahidi kupyaisha karama na kuimwilisha katika mazingira yanayowazunguka, ili jamii iweze kuboreshwa kwa chachu ya Injili. Hii ndiyo neema ambayo Mama Kanisa anaomba kwa ajili ya watawa katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linaendelea kukazia kwa namna ya pekee kabisa umuhimu wa kuzingatia na kuishi useja kama kielelezo cha ushuhuda wa uaminifu kwa Mungu na Kanisa kama sehemu ya ushiriki wao katika kazi ya ukombozi, ili kamwe asiwepo mtu anayepotea bila kupata wokovu. Nadhiri za ufukara na utii ni kielelezo cha ushuhuda dhidi ya ubinafsi unaotawala na kushika hatamu.

Watawa wajifungamanishe na Kristo katika maisha yao, kwa ajili ya jirani zao, huku wakionesha unabii, kwa ajili ya mafao ya wengi pamoja na kukaribisha tofauti zinazojitokeza ambazo kimsingi ni zawadi ya Roho Mtakatifu. Ulimwengu unaonekana kuwa umegawanyika katika makundi ya wale "wenye nacho na akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi", kumbe ni wajibu wa watawa kushuhudia moyo wa sadaka, ukweli na mapendo yanayojikita katika huduma.

Watawa katika maisha na utume wao, washuhudie ubinadamu uliopyaishwa kwa njia ya Yesu Kristo, tayari kujisadaka bila ya kujibakiza, ili kuwaendea maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; hawa ndio wale waliopotea na kujeruhiwa. Watawa wawasaidie watu hawa kung'amua utu na heshima yao; kwani wote hawa wanakumbatiwa na upendo wa Mungu unaojionesha kwa njia ya upendo unaobubujika kutoka ndani ya Kanisa.

Familia ya Mungu inakumbushwa kwamba, Mwaka wa Watawa ni kwa ajili ya waamini wote na wala si kwa watawa peke yao. Waamini wachukue fursa hii pia kufanya toba na wongofu wa ndani, tayari kupokea na kutumia neema na baraka zinazotolewa na Mama Kanisa katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani. Waamini walei waoneshe umoja na uwajibikaji katika kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu. Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linawatakia kheri na baraka watawa wote katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, waendelee kuonesha jeuri ya kujisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.