2015-01-28 12:12:06

Familia zinasambaratika!


Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara, katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha umuhimu wa mshikamano wa dhati katika maisha ya ndoa na familia kwa kutambua kwamba, familia ni mahali pa kutakatifuza maisha ya mwanadamu, shule ya kwanza upendo, haki na amani. RealAudioMP3

Familia ni mahali pa kurithisha tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu; yote haya yanawezekana ikiwa kama wazazi wa pande zote mbili wanatekeleza dhamana na wajibu wao wa kulea na kuwafunda watoto wao!

Askofu Niwemugizi anasema kwamba, familia nyingi nchini Tanzania zinakabiliwa na changamoto mbali mbali za maisha hususan katika uwanja wa malezi bora; dhamana inayopaswa kutekelezwa na wazazi wa pande zote mbili, lakini leo hii kuna familia nyingi ambazo ni tenge, yaani kuna mzazi mmoja anayewajibika katika yote, hali ambayo inakwamisha malezi kwa watoto.

Hali ngumu ya maisha imepelekea familia nyingi kujikuta zinaogelea katika lindi la umaskini wa hali na kipato, kiasi hata cha kushindwa kutekeleza dhamana na wajibu wake wa kulea na kuwafunda watoto; wazazi wengi wanashindwa kuzihudumia familia zao kwa kuzipatia mahitaji msingi, matokeo yake ni baadhi ya wazazi, hasa akina baba kutelekeza familia zao na "kuishia mitini".

Baadhi ya familia zinashindwa kujitosheleza kwa mahitaji yake msingi na matokeo yake, watoto wanalazimishwa kufanya kazi ambazo ni ngumu ikilinganishwa na umri wao, kiasi cha kuwadumaza katika makuzi yao. Baadhi ya wazazi wamekuwa ni chanzo cha kuwatumbukiza watoto wao katika biashara mamboleo, ili kusaidia kuchangia gharama za maisha kwenye familia, matokeo yake ni mimba za utotoni, ongezeko la ugonjwa wa Ukimwi pamoja na vifo.

Ukosefu wa mshikamano na mfungamanisho wa maisha ya ndoa na familia pamoja na sababu nyingi, watoto wengi wamejikuta wakiishi katika mazingira hatarishi. Zote hizi ni changamoto zinazoendelea kuikabili Familia ndani na nje ya Tanzania. Kuna haja kwa Mama Kanisa kuibua mbinu mkakati utakaoziwezesha familia kufungamana na hatimaye, kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa na Jamii kwa ujumla, hasa wakati huu, Mama Kanisa anapijielekeza katika mchakato wa kuwatangazia Watu wa Mataifa, Injili ya Familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.