Kanisa litakianza kipindi cha Kwaresima hapo tarehe 18 Februari 2015 kwa kupakwa majivu,
mwaliko wa kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu. Ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa kipindi
cha Kwaresima kwa mwaka 2015 unaongozwa na kauli mbiu "Imarisheni mioyo yenu" kwa
kutambua kwamba, kila mtu anapendwa na Mwenyezi Mungu na anamfahamu kila mtu kwa jina
na hata pale mwanadamu anapokengeuka, Mungu bado anamtafuta.
Baba Mtakatifu
Francisko anawachangamotisha waamini kuupokea na kuukumbatia upendo wa Mungu unaowatangulia
daima kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye aliyeanza kwanza kumpenda binadamu
na anaendelea kuliimarisha pendo lake na kwamba, ni wajibu wa waamini kuhakikisha
kwamba, wanawasaidia jirani zao, kwa kuwashirikisha upendo ambao wamejichotea kutoka
kwa Mungu na kuwawekea mbele yao, ili kuwahudumia hasa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii.
Baba Mtakatifu anasema katika ujumbe wake wa Kwaresima
kwa mwaka huu kwamba, pale ambapo mwanadamu anaishi kwa raha mustarehe, anakuwa na
kishawishi cha kuwasahau jirani zake wanaoteseka; katika shida na mahangaiko yao na
kwa kutotendewa haki. Katika mazingira kama haya, moyo wa mwanadamu unatumbukia katika
hali ya kutoguswa na mahangaiko yao, kishawishi kikuu kinachotoka kwa Shetani ambaye
anaendelea kujiinua hadi amepata utambulisho wa kimataifa.
Hapa Baba Mtakatifu
anazungumzia tabia ya ubinafsi kama utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko
ya wengine. Ni mtu yule tu ambaye aliwezeshwa kusafishwa miguu na Yesu anaweza kuwa
ni sehemu yake kwa kushiriki kikamilifu katika kuwahudumia jirani zake. Lakini kwa
wale wanaoelemewa na ubinafsi wao, wanajifungia ndani mwao, kiasi cha kushindwa kuwahudumia
jirani zao.
Wakristo wanapaswa kutambua na kuonja upendo mkamilifu ulioneshwa
na Yesu mwenyewe aliyejitaabisha kuinama na kuwaosha mitume wake miguu; ni kielelezo
cha pendo kuu ambalo Yesu analionesha kwa umaskini wa binadamu. Kuna haja kwa waamini
kujiachilia mikononi mwa Yesu, ili aweze kuwaosha miguu, yaani kuonja upendo wake
unaoponya licha ya mapungufu yanayoweza kujitokeza katika kumpenda Kristo. Watu wanaweza
kuonja upendo huu, kwa njia ya Kanisa na ndani ya Kanisa Mkristo anaweza kumwachia
Mwenyezi Mungu kumvika wema na huruma yake na hivyo kumwezesha kuwa na uwezo wa kuwaosha
wengine miguu yao; kwa kujisadaka kwa ajili ya Mungu na binadamu.
Baba Mtakatifu
Francisko anawaalika Wakristo kujenga na kudumisha moyo wa upendo na mshikamano wa
dhati, ili kuachana na utamaduni usioguswa na shida pamoja na mahangaiko ya watu,
kwa kutambua kwamba, wote ni viungo vya Fumbo la mwili huo mmoja, yaani Kanisa. Kila
aliye wa Kristo ni sehemu ya Fumbo la Mwili wake, kumbe hapaswi kuwageuzia jirani
zake kisogo. Baba Mtakatifu anasema... "na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia
nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho."
Hii
ndiyo dira ambayo Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuionesha katika maisha ya Jumuiya
na Parokia mbali mbali. Anauliza maswali ya msingi, ikiwa kama wanajumuiya wanajisikia
kuwa ni sehemu ya mwili huo mmoja? Mwili ambao kwa pamoja unapokea na kushirikishana
kile ambacho Mwenyezi Mungu amewakirimia katika maisha. Mwili unaotambua na kuwawajibikia,
maskini, wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Au wote wanajifunika
katika "blanketi" la upendo wa juma kwa kujishughulisha na malimwengu kwa kumsahau
Lazaro ambaye ameketi pembeni mwa mlango wao uliofungwa?
Baba Mtakatifu anawaalika
Wakristo kumwilisha upendo katika uhalisia wa maisha yao, kwa kushikamana na Kanisa
la mbinguni kwa njia ya sala, ili kujenga na kuimarisha mahusiano kati ya Kanisa linalosafiri
hapa duniani na Kanisa la mbinguni; umoja unaojikita katika huduma na mafao ya wengi
na kuhitimishwa kwa kumfahamu Mwenyezi Mungu. Kanisa linalosafiri na Kanisa la mbinguni
yanashirikiana ili kuhakikisha kwamba, hakuna mtu duniani ambaye anateseka au kuomboleza,
ili furaha ya ushindi wa Kristo Mfufuka iweze kufika hata mbinguni kama anavyosema
Mtakatifu Theresa wa Lisieux.
Kwa upande mwingine anasema Baba Mtakatifu Francisko,
Kanisa kwa asili ni la Kimissionari na kwamba, linatumwa kwa watu wote na kamwe lisijitafute
lenyewe na kwamba, Jumuiya ya Kikristo inachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha
kwamba, inavuka mahusiano yanayojikita katika jamii inayowazunguka, kwa kuwaangalia
maskini na wale walioko mbali zaidi.
Jitihada hizi zinapaswa kutekelezwa na
kila mwamini mmoja mmoja, kwa kushinda kishawishi cha kuwageuzia wengine kisogo kwa
njia ya sala, matendo ya huruma, ili daima mioyo ya waamini iendelee kumwongokea Mwenyezi
Mungu ambaye ni mwenye nguvu, mwingi wa huruma, makini na mkarimu, ambaye hawezi kujifungia
ndani mwake!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.