2015-01-26 08:51:10

Yatakatifuzeni malimwengu!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, mwishoni mwa juma, tarehe 24 Januari 2015 ametembelea na kuadhimisha Ibada ya Misa takatifu katika Jimbo Katoliki la Xuan Loc, ambalo lilianzishwa kunako tarehe 14 Oktoba 1965 na Mwenyeheri Paulo VI, ili kurahisisha huduma za kichungaji kwa waamini waliokuwa wanaongezeka kwa kasi kubwa.

Kumbe, Ibada hii ya Misa Takatifu, ilikuwa ni kilele cha maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Jimbo hili lililipoanzishwa. Katika kipindi cha miaka mitano ya maandalizi ya Jubilee, familia imepewa kipaumbele cha kwanza, katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kuhakikisha kwamba, familia inakuwa kweli ni shule ya Neno la Mungu na kwamba, Familia zinajichotea nguvu na neema ya kusonga mbele katika Sakramenti za Kanisa; kielelezo cha mshikamano wa dhati kati ya Wakleri na waamini walei.

Mama Kanisa anasema Kardinali Filoni anaendelea kuwachangamotisha waamini nchini Vietnam kusonga mbele kwa kujikita katika mchakato wa Uinjilishaji mpya unaofumbatwa katika ushuhuda wa imani katika matendo. Ikumbukwe kwamba, Jimbo Katoliki la Xuan Loc ni matunda ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, linalotegemewa kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji wa Familia ya Mungu kama Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanavyokazia.

Ni dhamana ya kuhakikisha kwamba, Familia ya Mungu inajitahidi kupyaisha imani inayojikita katika matendo yanayoshuhudiwa katika uhalisia wa maisha ya waamini, daima wakijitahidi kuwa kweli ni waaminifu kwa Mungu na Kanisa, wakiendelea kukumbatia Injili ya Huruma ya Mungu ili kuwatangazia jirani zao matendo makuu ya Mungu katika maisha yao. Familia ya Mungu, iwaonjeshe wengine huruma na upendo wa Mungu kwa kuwatangazia Habari Njema ya Wokovu na kutangaza Mwaka wa Bwana.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.