2015-01-26 08:42:59

Umoja wa Wakristo!


Yesu alianza kuhubiri Habari Njema ya Wokovu mara baada ya Yohane Mbatizaji kufungwa gerezani na Mfalme Herode. Huu ulikuwa ni wakati ambapo sauti ya kinabii ilikuwa inaanza kutangaza kuhusu Ufalme wa Mungu, lakini Mfalme Herode akamua kuizima. Yesu ndiye kiini na Habari Njema, utilimifu wa maagano kati ya Mungu na mwanadamu; ndiye Habari Njema inayopaswa kuaminiwa, kupokelewa na kutangazwa kwa Watu wa nyakati zote, ili aweze kuaminiwa na wote.

Hii ni sehemu ya tafakari iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, siku ya Jumapili tarehe 25 Januari 2015, siku ya kufunga juma la kuombea Umoja wa Wakristo.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu Kristo ni Neno wa Mungu aliye hai na anayetenda katika historia, kwa mtu anayemsikiliza na kumfuasa anaingia kwenye Ufalme wa Mungu. Yesu ni utimiliufu wa ahadi za Mungu kwani anawakarimia waja wake Roho Mtakatifu. Yesu ni maji hai yanayozima kiu ya moyo wa mwanadamu unaohitaji: maisha, upendo, uhuru na amani; ni moyo wenye kiu ya Mungu. Ndiyo maana kauli mbiu iliyoongoza juma la kuombea umoja wa Wakristo kwa Mwaka huu, ilikuwa “nipe maji ninywe”.

Baba Mtakatifu anasema, Kanisa bado linaendelea kumwomba Kristo ili aweze kulipatia nguvu na dhamana ya kutafuta umoja kamili kati ya Wakristo, ili wote waweze kuwa wamoja. Dhambi za Wakristo na historia yao, imekuwa ni chanzo cha utengano, ndiyo maana Wakristo wanapaswa kuendelea kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze kuwajalia tena umoja.

Baba Mtakatifu anasema, kwa njia ya Fumbo la Umwilisho, Mwenyezi Mungu amekuwa ni kiu ya binadamu anayetaka utimilifu wa maisha yasiyojikita katika utumwa wa dhambi na mauti. Kwa hakika, Mwenyezi Mungu ana kiu na upendo wa mwanadamu unaojikita katika Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambao kimsingi ni daraja kati ya kiu ya Mungu na mwanadamu. Yesu anataka kuunganisha, lakini Shetani daima amekuwa ni chanzo cha migawanyo, chuki na vita.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.