2015-01-26 09:04:29

Uekumene wa damu!


Yesu katika maisha na utume wake, kamwe hakusita kukutana na kuzungumza na watu ambao walikuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii, kiasi hata cha kukutana na kuzungumza na mwanamke Msamaria na hivyo kuanzisha majadiliano yaliyopelekea hija ya toba na wongofu wa ndani. Yesu alionesha uvumilivu mkuu na kumheshimu yule mwanamke Msamaria. Akawa tayari kujifunua kwake taratibu kama mawio ya jua, kwa kujikita katika upendo na ukweli; kwa kuonesha ukarimu sanjari na kusikiliza kwa makini. Umoja wa Wakristo unajengeka kwa njia ya hija ya maisha ya Wakristo pasi na kukata tamaa!

Hayo yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri kwenye Masifu ya Jioni, Siku kuu ya kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, Mtume wa mataifa na siku ya mwisho ya kufunga sala kwa ajili ya juma la kuombea umoja wa Wakristo. Mwenyezi Mungu anasema Baba Mtakatifu kadiri ya Maandiko Matakatifu anapaswa kuabudiwa katika roho na ukweli. Leo hii, bado wakristo wamegawanyika kutokana na historia waliyorithi huko nyuma, changamoto ya kuvuka vikwazo vyote hivi na kuanza mchakato wa kushiriki katika Fumbo la Upendo linalojikita katika Utatu Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anasema umoja wa Wakristo hauwezi kujengwa kwa majadiliano ya kiekumene peke yake, bali Wakristo wanapaswa kutambua kwa kina Fumbo la Mungu na kwamba, wanategemeana, kumbe Wakristo wanaweza kukutana na kujadiliana kwa pamoja chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu, anayesawazisha tofauti na kushinda kinzani, ili kupatanisha tofauti zinazojitokeza.

Yesu anajionesha kuwa ni chemchemi hai inayozima kiu ya maisha ya mwanadamu; kiu ambayo inajikita katika ukweli, upendo, haki na uhuru na kwamba, kwa njia ya Fumbo la Pasaka, Yesu anakata kiu yote ya maisha ya binadamu, pale Moyo wake Mtakatifu unapotobolewa na hivyo kutoa Damu na Maji, kielelezo cha hali ya juu cha upendo wa Mungu kwa binadamu, changamoto ya kujenga na kudumisha umoja wa Watoto wa Mungu, unaojikita katika unyenyekevu wa Kristo.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu kwa kukutana na Mwanamke Msamaria, anamsaidia kuwa Mmissionari, anaacha yote aliyokuwa nayo pale kisimani na kuanza kutimua mbio kwenda mjini ili kuwashirikisha wengine ile furaha ya kukutana na Yesu katika maisha yake. Leo hii kuna kundi kubwa la watu waliochoka na wenye kiu ya kumwona Mungu, changamoto ya kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji, kwa Makanisa kushirikiana kwa karibu zaidi pamoja na kuvuka kishawishi cha kutaka kuwaongoa watu na mashindano yasiokuwa na tija wa la mashiko.

Baba Mtakatifu anasema, kuna Wakristo wanaoendelea kudhulumiwa, kunyanyaswa na hatimaye kuuwawa kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Hawa ni mashuhuda wa Kristo, wanauwawa hata pasi ya kuulizwa wanatoka katika madhehebu gani; wanauwawa kwa vile ni Wakristo, huu ndio uekumene wa damu.

Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwapongeza wawakilishi mbali mbali wa madhehebu ya Kikristo walioshiriki katika Ibada ya kufunga rasmi juma la kuombea umoja wa Wakristo bila kuwasahau watawa kutoka katika Makanisa mbali mbali waliokuwa wanashiriki katika kongamano la Mwaka wa Watawa Duniani mintarafu mchakato wa majadiliano ya kiekumene. Watawa wa madhehebu mbali mbali ya Kikristo wanapaswa kufahamiana na kushirikishana uzoefu, ujuzi na mang'amuzi, ili kuendelea kulipyaisha Kanisa.

Baba Mtakatifu anasema,Wakristo wana kiu ya amani na udugu, changamoto ya kuendelea kuliomba Fumbo la Utatu Mtakatifu, Bikira Maria, Mitume na Watakatifu wote, ili Wakristo waweze kupata zawadi ya umoja, ili kweli Fumbo la Umoja wa Kanisa liweze kung'ara.

Naye Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la kuhamasisha umoja wa Wakristo, amemwambia Baba Mtakatifu kwamba, Wakristo wa madhehebu mbali mbali wamekusanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, nje ya kuta za Roma, ili kuomba maji ya uzima wa milele, kwa kutambua kwamba, kwa njia ya Maji ya Ubatizo, Wakristo wamefanywa kuwa wamoja katika Yesu Kristo na kwamba, Ubatizo ni Sakramenti ya Umoja na amani, ili kuvuka chuki, kinzani na vita. Wakristo wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa kweli ni vyombo vya amani na upatanisho, mwaliko wa kutubu na kumwongokea Kristo, tayari kuwa Wamissionari wa Kristo kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Paulo, Mwalimu wa Mataifa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.