2015-01-26 08:44:36

Mshikamano na wagonjwa wa Ukoma!


Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 25 Januari 2015, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Baba Mtakatifu Francisko anasema, anaendelea kufuatilia kwa wasi wasi mkubwa machafuko ya kisiasa yanayoendelea kutendeka nchini Ucrain; mambo ambayo yanaendelea kusababisha umwagaji wa damu ya raia wasiokuwa na hatia.

Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wote kwamba, yuko karibu nao kwa njia ya sala na anapenda kutoa mwaliko kwa wahusika wakuu, kuanzisha tena mchakato wa majadiliano ili kusitisha chuki, uhasama na vita vinavyoendelea nchini humo.

Baba Mtakatifu Francisko, amewakumbusha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwamba, Jumapili, ilikuwa ni Siku ya Wagonjwa wa Ukoma Duniani. Anapenda kuonesha uwepo wake wa karibu kwa wagonjwa wa ukoma, wale wanaowahudumia pamoja na wataalam wanaoendelea kujisadaka mchana na usiku ili kuweza kupata tiba ikayaoweza kuwarudia wagonjwa wa ukoma hadhi yao.

Baba Mtakatifu Francisko, amewashukuru kwa namna ya pekee kabisa Jumuiya ya wananchi wa Ufilippini, waliokuwa wamekusanyika kwa wingi wakiwa wanapeperusha bendera ya nchi yao, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Baba Mtakatifu anawashukuru kwa ushuhuda wa imani na kazi kubwa wanayoitenda kwa wakazi wa Roma.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.