2015-01-26 08:46:23

Mradi wa maji Burkina Faso


Vijana wanapaswa kufundwa kuwapenda na kuwathamini jirani zao kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu. Jumapili iliyopita, tarehe 25 Januari 2015, wanachama 3, 000 wa Chama cha Vijana Wakatoliki Italia, A.C.R. walifanya maandamano ya kuombea amani sehemu mbali mbali za dunia na baadaye nyakati za mchana kuhudhuria kwenye Sala ya Malaika wa Bwana, iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Kauli mbiu ya mwaka huu ni "Changia amani".

Vijana hao katika ujumbe uliosomwa kwa niaba yao na kijana Sara wamemwambia Baba Mtakatifu Francisko kwamba, wana kiu ya amani, furaha na utulivu wa ndani unaopata chimbuko lake kutoka kwa Kristo na kwamba, kila mwaka walezi wao wanajibidisha kuwafunda mbinu za kujenga, kulinda na kudumisha amani, kwa kuchota uzoefu wao kutoka katika hekima, lakini zaidi katika Maandiko Matakatifu.

Vijana wamekusanya fedha kwa ajili ya kugharimia mradi wa maji utakosaidia wananchi wengi vijijini nchini Burkina Faso. Maji haya pamoja na matumizi ya nyumbani yatasaidia pia katika kilimo cha umwagiliaji, ili kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.