2015-01-26 11:30:22

Elimu ni bahari!


Familia ya Mungu nchini Tanzania imeshauriwa kuendelea kujituma na kuwekeza zaidi katika elimu ili iweze kulitumikia vyema Kanisa mahalia kwa kutumia kikamilifu karama walizokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa kutambua kwamba, elimu haina mwisho.
Wito huo umetolewa hivi karibuni na Padre Sebastian Mwaja ambaye ni Paroko wa Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo kuu la Dodoma, wakati wa hafla fupi ya kumpongeza Padre Abel Mwenda na mwanafunzi mwenzake Alpha Muhulo kwa kuhitimu shahada ya elimu katika Chuo kikuu huria mjini Dodoma.
Paroko Mwaja amesema elimu ni urithi na mtaji pekee wa kujivunia na kwamba endapo waamini, watawa na Wakleri watajituma katika kujiendeleza, Kanisa litaendelea kudumu katika misingi yake itakayokuwa inaendelea kwa kasi kutokana na kila mmoja kuchangia karama yake katika kuliendeleza Kanisa mahalia.
“Mimi nakupongeza sana Baba Padre Abel kwa kujituma na kuonesha jihada za kujiendeleza pamoja na mwenzako hadi mmehitimu, ni tukio la kipekee ambalo kila mmoja wetu katika Jimbo kuu la Dodoma tuna kila sababu ya kusherehekea na kujivunia,” alisema.
Kwa upande wake, Padre Abel Mwenda amewashukuru mapdre na masista kwa kumtia moyo katika kipindi chote cha masomo na kwamba, waendelee na moyo huo kwa wengine huku Apha Muhulo akimshukuru Padre kwa kusaidiana naye katika dhiki na faraja hadi wamehitimu shahada ya kwanza ya elimu.
Na Thompson Mpanji,
Dodoma.








All the contents on this site are copyrighted ©.