2015-01-24 08:17:35

Papa aguswa na mahangaiko ya wananchi wa Malawi!


Baba Mtakatifu Francisko ameiandikia Familia ya Mungu nchini Malawi, ujumbe wa upendo na mshikamano hasa wakati huu inapokabiliana na janga la mafuriko ambalo limeathiri maisha ya watu na miundo mbinu. Katika ujumbe uliotiwa sahihi na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwenda kwa Askofu mkuu Thomas Msusa wa Jimbo kuu la Blantyre, Malawi, Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wananchi wote wa Malawi walioguswa na mafuriko haya uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala.

Baba Mtakatifu anawaombea ujasiri na nguvu ya kukabilia na changamoto zilizopo kwa sasa na kwamba, anatumaini kuwa Jumuiya ya Kimataifa itawasaidia wananchi wa Malawi katika kipindi hiki kigumu. Anawatakia kheri na baraka wafanyakazi wote wanaoendelea kutoa huduma mbali mbali kwa waathirika wa mafuriko yaliyotokea hivi karubuni nchini Malawi.

Wakati huo huo, Rais Peter Mutharika wa Malawi ametangaza kwamba, kuna Wilaya kumi na tano ambazo zimekumbwa na mafuriko na zinahitaji msaada wa dharura. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu 200 ambao wamefariki dunia na wengine wengi hawana mahali pa kuishi kutokana na mafuriko yaliyotokea nchini Malawi. Kuna zaidi ya watu 200, 000 hawana makazi na kwamba, makazi ya watu, shule na miundo mbinu imeharibiwa sana.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.