2015-01-24 12:16:55

Msichochee ghasia kwa kampeni chafu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria linapenda kuwapongeza wanasiasa na wananchi wote ambao hadi wakati huu wameendesha kampeni zao kwa kuzingatia misingi ya haki, amani na utulivu na kwamba, wanapaswa kuendelea katika mwelekeo huu, ili kweli cheche za matumaini ya amani na utulivu ziweze kurejea tena nchini humo, ambako kuna watu wanateseka kutoka na mashambulizi ya mara kwa mara yanayofanywa na Kikundi cha Boko Haram.

Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria limeyasema haya katika mkutano wake wa mwanzo wa Mwaka, uliofanyika hivi karubuni mjini Ibadan. Wanasikitika kusema kwamba, kuna baadhi ya wanasiasa wanaoendesha kampeni zao kwa kupandikiza chuki na uhasama kati ya watu, ili kutafuta kura kwa nguvu, jambo ambalo ni hatari kwa umoja na mshikamano wa kitaifa.

Maaskofu Nigeria wanaitaka Serikali kuhakikisha kwamba, inalivalia njuga tatizo la Boko Haram ambalo kwa sasa ni tishio la kimataifa na chanzo cha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia. Maaskofu wanasema, Kanisa kwa upande wake, litaendelea kutangaza Injili ya Uhai, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu. Maaskofu wanawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Nigeria kusimama kidete kupinga utamaduni wa kifo, udini, ukabila na umajimbo. Wazazi wawajibike kikamilifu katika maisha ya ndoa na familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.