2015-01-23 12:11:09

Bikira Maria linda kazi na matunda ya Uinjilishaji!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, Alhamisi, tarehe 22 Januari 2015 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria Mama wa Mungu wa La Vang, nchini Vietnam, kwa kumwomba Bikira Maria kulinda kazi na matunda ya mchakato wa Uinjilishaji sehemu mbali mbali za dunia.

Bikira Maria ni Mama wa Neno wa Mungu, Injili Hai, aliyethubutu kumsindikiza Mwanaye Mpendwa, Yesu Kristo katika hija ya maisha yake hapa duniani na wakati wa Pentekoste, akashuhudia Kanisa likizaliwa na kuanza kuenea sehemu mbali mbali za dunia, leo hii Injili imefika hata Vietnam.

Kardinali Filoni anasema, Bikira Maria ni Mama mwenye ujasiri, aliyediriki kusimama chini ya Msalaba, akakubali kupokea dhamana ya kuwa ni Mama wa wote, tangu wakati ule. Bikira Maria ameendelea kuwa kweli ni Mama wa wote, kielelezo kwamba, Yesu alipenda kuwazawaidia wafuasi wake Bikira Maria, ili aweze kuwa kweli ni msaada na mwombezi katika hija ya maisha yao. Bikira Maria anaendelea kuwa ni kielelezo cha uwepo wake endelevu katika Madhabahu mbali mbali duniani, kama vile: Lourdes, Fatima na La Vang, nchini Vietnam.

Hapa palikuwa ni kimbilio la waamini walipokumbana na madhulumu na nyanyaso za kidini, wakapata ulinzi na tunza ya Bikira Maria, ndiyo maana haya ni Madhabahu ya kitaifa, mahali pa kukutana, kusali, kutafakari na kuomba ulinzi na tunza ya Bikira Maria. Kardinali Fernando Filoni, kwa niaba ya Familia ya Mungu nchini Vietnam, amemshukuru Yesu Kristo kwa kuwazawadia zawadi ya Bikira Maria na kwamba, anamwomba aendelee kusaidia mchakato wa Uinjilishaji mpya Barani Asia.







All the contents on this site are copyrighted ©.