Tafakari ya Neno la Mungu Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican kipindi Tafakari Neno la Mungu, leo tunaangalia
maisha yetu tukiongozwa na Neno la Mungu lililo chimbuko ya furaha yetu. Ni Dominika
ya tatu ya mwaka wa Kanisa. Ujumbe tunaopaswa kuubeba mioyoni mwetu ni Toba na kuitikia
wito utokao kwa Mungu.
Katika somo
la kwanza tunamwona Nabii Yona anaitwa na Mungu ili kutangaza habari ya toba kwa mataifa.
Yona anajitahidi kukwepa mwaliko wa Mungu lakini Mungu aliye mwaminifu katika uamuzi
wake hakati tamaa mpaka Yona atakapokubali mwaliko wake. Baada ya kukubali mwaliko
wa Mungu nabii Yona anakwenda Ninawi kutangaza ujumbe wa Mungu unaowaalika watu kutubu
katika kipindi cha siku arobaini vinginevyo anaangamiza mji huo.
Basi watu
wa Ninawi wakijua upendo wa Mungu na hukumu zake kuwa ni za haki wanaitika wito wa
toba, wanajivika mavazi ya magunia, alama ya toba na wanabadilisha maisha yao. Kwa
sababu Mungu hubaki mwaminifu katika ahadi zake anaghairi angamizo ambalo angelitenda
kwa Ninawi.
Mpendwa, yako mambo mengi ya kujifunza katika hili kwanza wakati
fulani inatokea katika maisha yetu tunakataa wito wa Mungu wa toba na hata wa kwenda
kutangaza habari njema. Kumbe yafaa kuangalia kwa makini ili tusije tukapoteza nafasi
ya wokovu kwa sababu ya kukataa mwaliko wa toba na wito wa kimisionari. Kumbukeni
Kanisa letu kwa asili ni la kimisionari. Twajifunza kuwa bidii kidogo tu katika kubadilisha
mwenendo wetu mbaya yamfanya Mungu aghairi nia yake.
Mtume Paulo anapowaandikia
Wakorinto yuko katika mtindo uleule wa kuweka maisha yetu mikononi mwa Mungu. Kuitika
daima upendo wa Mungu na hivi kutumia mali ya dunia kama chombo cha kutusaidia kujenga
mahusiano mazuri na Mungu mwenyezi. Anawaambia kuwa muda tulionao hapa duniani ni
mfupi na hivi tuutumie vema kwa ajili ya toba na hivi kuambatana na mapenzi ya Mungu.
Wazo
la toba na wito linajitokeza waziwazi katika Injili ya Marko. Toba ni mwanzo wa Injili
ya Marko pale tunaposikia tubuni na kuiamini Injili (Mk 1:15) Bwana anataka watu watubu
ili watoe nafasi mioyoni mwao kwa ajili ya upendo wa Mungu. Bila toba na kuamini,
mmoja hawezi kupokea habari njema. Ndiyo maana Kanisa husisitiza waamini wapokee daima
sakramenti ya kitubio njia ya neema za Mungu.
Sehemu ya pili ya Injili ya
dominika hii ni juu ya ni wito wa Mitume. Bwana anawaita mitume wamfuate na wafanye
kazi ya toba na wasaidie kazi ya wokovu. Katika kuwaita yapo mambo ambayo yafaa kuyaangalia.
Kwanza wito ni zawadi na pili ndani ya wito kuna Msalaba.
Tunamwona Bwana
akiwaita Mitume wakati huohuo yuko kazini, yuko njiani, hasimami na kuanza kuwabembeleza
bali anasonga mbele, kwa maana hiyo nasi hatukuitwa ili kubembelezwa bali kushika
njia ya Bwana inayoambatana na umisionari, wajibu na mateso ndani yake. Ndiyo kusema,
kumfuasa Bwana si kwenda likizo bali kukaza moyo na kuishi mapenzi ya Mungu. Wanaoitwa
wanaacha kila kitu pamoja na wazazi wanaanza safari ya wokovu. Wanaitika wito kama
watu wa Ninawi ambao mara moja wameitika na kubadili maisha yao.
Mpendwa unayenisikiliza
yakupasa kujenga utamaduni wa toba ili kwa njia hiyo basi ukomavu wa wito uliokabidhiwa
siku ya ubatizo wako utakuwa siku kwa siku ukiongezeka.
Ninakutakieni heri
na baraka za Mungu katika kushika na kutenda mapenzi ya Mungu ambapo watakiwa kwanza
kutubu na kisha kuanza safari bila kuwazawaza mambo ya jana au ya kidunia bali yaliyo
ya kimungu.
Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard
Tiganya C.PP.S.