2015-01-21 09:14:03

Ilani!


Tangazo maalum: “Muda umefika na wakati ni huu wa kufanya mapinduzi na kuingiza utawala mpya!” Ninaposema muda au wakati simaanishi muda wa saa ya mkononi ambayo wagiriki wanaita kronos, la hasha, bali ni muda ambao wanaita kairos, yaani wakati mwafaka, wakati utakiwao. Muda mwafaka wa kufanya mapinduzi ndiyo huu, ukikosa kufanya mageuzi sasa basi “itakula kwako.” Mapinduzi hayo ni ya serikali, ya siasa, ya dini, ya kiroho, ya kimaadili kwa ulimwengu mzima. Utekelezaji wa tangazo hilo mtaushuhudia.


Hebu nikudokezee kwa kifupi mazingira yalivyoandaliwa ya mapinduzi hayo. Leo utashuhudia jinsi vituko vilivyojipangana pamoja katika mchakato huo wa mapinduzi. Mosi, tutamshuhudia bwana mmoja aliyekuwa amemnadisha na kumtangaza sana huyo mleta mapinduzi ametiwa gerezani, pili, Mwanamapinduzi mwenyewe utamwona anatembea kwa uhuru wote huku na huku barabarani akitafuta wafuasi, anatembelea ufuoni mwa ziwa, anaona mashua, anaona nyavu na wavuvi na anawaita kumfuata, nao wanatelekeza nyavu na baba zao wanainuka kumfuata. Hii ndiyo kasi mpya anayoanza nayo, yaani kupita kujinadisha na kutangaza adhima yake ya mapinduzi anayotaka kuyafanya ya kutaka kuingiza utawala mpya.


Tuanze kuviona vituko hivyo kimoja baada ya kingine: “Baada ya Yohane kutiwa gerezani, Yesu akaenda Galilea kufundisha.” Maana yake, hata kama Yohane aliyembatiza na kumtangaza Yesu amenyamazishwa kwa kutiwa gerezani, Neno jipya linachukua kasi yake mara moja. Yesu, anazunguka vijijini kuanza kampeni zake. Haanzi kazi mjini Yerusalemu, kwenye hekalu kubwa na makuhani wakuu, na wakuu wa serikali na siasa, bali anaanza kijijini huko Galilea ya upagani, kwa watu mchanganyiko waliodharauliwa tena katika Sinagogi au kigangoni.


Huko anaanza kutoa tangazo la mapinduzi: “Wakati umetimia, Utawala wa Mungu umekaribia; Ongokeni na kuamini Injili,” ni wakati mwafaka wa kufanya mapinduzi kwa maisha mazima ya binadamu. Maana yake, wale waliojulikana kuwa watu wa maana hapa duniani kutokana na utajiri wao, basi sasa ndiyo mwisho wa habari. Wale wenye kuheshimika kutokana na utajiri sasa watakuwa maskini. Wakuu wanashushwa na wanyonge wanapandishwa. Hayo ni mapinduzi ya kweli kwani watu wanarudishiwa thamani ya utu wao.


Halafu “Utawala wa Mungu umekaribia” hayo ni maneno ya kimapinduzi yaonekana kama yanashuka kutoka mbinguni hadi duniani, toka kwa Mungu hadi kwa binadamu, yaani ufalme huu unatoka mbinguni, Mungu anajitokeza kama binadamu. Mungu anataka binadamu awe binadamu inavyotakiwa kuwa siyo mnyama. Kumbe maneno “Ongokeni na kuamini Injili” yanaonesha kupanda toka binadamu kwenda juu mbinguni, yaani ni wajibu wa binadamu kwa Mungu. Njia pekee ya kuongoka na kuwa binadamu ni “kuamini Injili” Yesu anasema: ongokeni, aminini, sadikini habari njema, msidanganyike na mambo mengine na watu wengine. “Aminini ninachosema mimi.” Yohane mbatizaji na manabii walionya kuwa, kama hamwongoki mtaadhibiwa. Lakini Yesu anataka kuongoka kule kwa kubadili fikra.


Mungu aliyejulikana kuwa anahifadhi wenye nguvu na ni mkali, mlipiza kisasi, hali iliyowakuza kichwa wafalme na watawala hao sasa ni tofauti yabidi kubadili fikra. Ama kweli Yesu ni mwana mapinduzi. Baadaye kidogo mtaona jinsi Yesu atakapoyafanya mapinduzi yenyewe pale atakapoponya, atakapotakasa, atakapofungua vizingiti vya milango, atakapopatanisha watu na wale waliotengwa na jamii.


Baada ya tangazo hilo la mapinduzi anapita kuchagua wafuasi wa kufanya naye kazi hiyo ya mapinduzi. Wafuasi hao hawachaguliwi kutoka katika mazingira ya kanisa, au mazingira ya kusali, bali ameamua kuwachagua katika mazingira ya ziwani, watu wakiwa katika kazi zao za kawaida za uvuvi, inamaanisha kwamba ufalme wa Mungu unaingia katika maisha ya watu wa kawaida.


Huko ziwani katika tembeatembea yake anamwona Simoni. Mara moja anafikiri kwamba huyu anaweza kuwa tofali la kwanza la ujenzi. Halafu anamwona Yohane na anagundua kuwa huyo ataweza kuwa na lugha ya kufaa kutangaza upendo. Baadaye zaidi anamwona hata malaya ambaye anaweza kupenda vizuri kuliko anavyofanya hadi sasa. Huo ndiyo mwono wake wa uumbaji mpya.


Kumbe, Bwana anaweza kuniona hata mimi labda nitaweza kushirikiana naye hapa ulimwenguni kwa kutumia mikono yangu kichwa changu na moyo wangu. Kisha anawaambia aliowaiga: “Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.” Kinyume cha mategemeo yao na yetu. Watu hawa walidhani mwito huu ni wa kupata cheo au kudokezewa kufanya kazi yenye kipato zaidi au kazi yao inaboreshwa, labda watafanya kazi ya utafutaji lulu au hazina ya thamani. Kumbe wanaambiwa zoezi la uvuvi linaendelea lakini sasa mtazamia ulimwenguni kote na kuvua watu.


Watu ndiyo wanaokuwa lulu na hazina, maana yake itawabidi kufanya juu chini kuwatafuta watu popote pale hao watu wanapojidhani wamefika kumbe hawajafika, pale wanapoona wamepata kumbe wamepatikana, au wanapoona wamestarehe na kuvuta hewa safi kumbe wamekaa karibu na shimo la choo wakivuta hewa chafu. Wafuasi yabidi waende wakawavue watu toka katika mazingira hayo ya ovyo na kuwaweka safi. Kwa hiyo Yesu amewaonesha wafuasi wake miondoko miwili ya kufuata. Mosi kufuata mgongoni pake na pili kuwaendea watu na kuwafundisha.


“Mara wakaziacha nyavu zao na kumfuata.” Wavuvi wanafahamu kazi ya nyavu ni kunasa samaki na kuwavua toka majini walimo huru. Samaki akinasa nyavuni hawezi kutoka kirahisi. Tukijiangalia kwa makini hata sisi wakati fulani tunajinasa na kukamatika katika nyavu mbalimbali za maisha. Tunavirigwa vibaya hata tunashindwa kujinasua. Wengine tunanaswa kwenye nyavu za ulevi, wengine kwenye ngono, wengine kwenye madaraka, wengine kwenye wivu, wongo, maraharaha, uvivu, hasira, pesa, utajiri nk. Huko tulikonaswa ndiko tunajisikia tumefika na hatutaki kutoka. Je, mwenzangu umenaswa kwenye nyavu zipi?


Huo ndiyo ukisikia ulimwengu wa kupagawa na pepo mchafu tutakayemsikia dominika ijayo. Aina nyingine ya nyavu zilizotuviriga na tunazopaswa kujinasua nazo ndizo zile tunazosikia pale wanapoitwa waana wa Zebedeo. Yasemwa, kwamba walipoitwa, “Wakamwacha baba yao mashuani pamoja na nyavu wakamfuata.” “Baba” yamaanisha mapokeo, na “Nyavu” ni desturi. Watoto hawa maram moja wakaachana na mambo ya kale waliyozoea, wakaachana na thamani za kale zinazopingana na mambo mapya. Nasi tuzikate nyavu zilizotunasa na tumfuate mwalimu huyu mwana mapinduzi na mwanakondoo katika safari yake. Wakati ni huu wa kufanya mapinduzi!


Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.