Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema katika kumbu kumbu ya miaka
sitini tangu alipozaliwa, Baba Mtakatifu Francisko amempatia zawadi kubwa kwa kushirikisha
furaha yake na ile furaha ya Familia ya Mungu nchini Ufilippini, walipokuwa wanakutana
na Wakleri, Watawa na Majandokasisi.
Anasema, hija ya Baba Mtakatifu Francisko
nchini Ufilippini, ilikuwa ni kiboko chake, hajawahi kuona umati mkubwa wa watu wakishiriki
kikamilifu katika mapokezi na maadhimisho mbali mbali ya Ibada zilizoongozwa na Baba
Mtakatifu Francisko. Hii inaonesha kwamba, kweli Familia ya Mungu nchini Ufilippini
ina upendo mkubwa kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro, Baba na Rafiki wa maskini. Amewatia
moyo watu waliotikiswa na janga la Yolanda na kwamba, wamejionea wenyewe mshikamano
na upendo wa kidugu ulioneshwa na wananchi wa Ufilippini pamoja na kutoka katika Jumuiya
ya Kimataifa.
Kardinali Parolin anasema, katika hija ya kitume ya Baba Mtakatifu
Francisko nchini Ufilippini, ameguswa kwa namna ya pekee na ushuhuda wa imani na matumaini
uliotolewa na vijana na familia walipokutana na Baba Mtakatifu; mambo ambayo yamemtajirisha
pia katika maisha na utume wake. Tufani ya Yolanda iliharibu miundo mbinu, lakini
imani ikabaki thabiti.
Kardinali Parolin anasema, hali ilikuwa ni tofauti kabisa
nchini Sri Lanka, ambako idadi ya Wakristo ni asilimia 6% ya idadi ya wananchi wote
wa Sri Lanka, lakini ni waamini walionesha moyo wa Sala na Ibada; upendo na mshikamano
na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Sri Lanka bado ina makovu ya vita ya wenyewe kwa wenyewe
iliyodumu kwa takribani miaka thelathini, changamoto kwa sasa ni kuganga na kuponya
madonda ya chuki na uhasama, tayari kujikita katika mchakato wa haki, amani, upatanisho,
msamaha na umoja wa kitaifa, kama ambavyo ameelezea Rais mpya wa Sri Lanka wakati
alipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko.
Kanisa linapenda kukazia
umuhimu wa mchakato wa upatanisho unaojikita katika ukweli na uwazi; upendo na mshikamano;
haki na msamaha wa kweli; ili wananchi waweze kuwa na ujasiri wa kuanza hija ya upatanisho
na umoja wa kitaifa. Ndiyo maana anasema Kardinali Parolin Madhabahu ya Madhu ni kielelezo
muhimu sana katika umoja, upatanisho na msamaha kati ya wananchi wa Sri Lanka. Hapa
ni mahali pa sala, msamaha na upatanisho kati ya waamini wa dini mbali mbali nchini
humo.
Kardinali Parolin anasema, Kanisa na watu wenye mapenzi mema wanalaani
kwa nguvu zote vitendo vya kigaidi, vita na mashambulizi yanayofanywa kutokana na
misimamo mikali ya kiimani. Ndiyo maana Baba Mtakatifu anawaalika viongozi wa dini
mbali mbali kukemea na kulaani kwa macho makavu vitendo vya kigaidi kwani ni tishio
kubwa kwa amani na usalama wa Jumuiya ya Kimataifa. Kanisa bado linapenda kuendeleza
mchakato wa majadiliano ya kidini ili kujenga na kuimarisha ushirikiano, umoja na
udugu miongoni mwa watu wa dini mbali mbali. Amani ya kweli inamwadabisha adui: kiroho
na kimwili anasema Mtakatifu Ignasi wa Antiokia.
Kardinali Parolin anasema,
kuna cheche za matumaini ya kuimarisha mahusiano kati ya Vatican na China, kwani kwa
mara ya pili sasa Baba Mtakatifu anapita katika anga la Jamhuri ya Wananchi wa China.
Kanisa linaendelea kusali na kujibidisha, ili siku moja, China na Vatican waweze kukutana
katika ukweli na upendo, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia ya Mungu nchini
China; katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, haki na amani.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.