2015-01-19 09:04:47

Watawa na majadiliano ya kiekumene!


Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 25 Januari 2015 yatafanyika kwenye Chuo kikuu cha Kipapa cha Mababa wa Kanisa cha Waagostiani, kilichoko mjini Roma. Haya ni maadhimisho ya kiekumene yanayoratibiwa na Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume.

Kanisa linatambua kwamba, majadiliano ya kiekumene ni sehemu ya mchakato wa maisha na utume wa Kanisa, mambo msingi yanayotekelezwa na watawa katika maisha na huduma zao kwa Familia ya Mungu. Hiki ni kielelezo makini cha Fumbo la Mwili wa Kristo yaani, Kanisa, safari makini ya kiekumene.

Maadhimisho haya yanafanyika wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuombea umoja wa Wakristo, kiasi kwamba, watawa kutoka Makanisa ya: Kikatoliki, Kiorthodox, Kianglikani na Kiluteri watashirikisha uzoefu na mang’amuzi yao katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene. Maadhimisho haya yatakuwa yanafungwa kwa Sala ya Masifu ya Jioni, muda wa saa 1: 00 Usiku, kwa saa za Ulaya.

Jumapili tarehe 25 Januari 2015, majira ya saa 11:30 za jioni, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Masifu ya Pili ya Jioni kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo nje ya kuta za Roma katika maadhimisho ya Siku kuu ya kuongoka kwa Mtakatifu Paulo. Baba Mtakatifu katika barua yake kwa watawa kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa anawahimiza watawa kukutana na kusali kwa pamoja na watawa wa Makanisa mengine ya Kikristo, ili kukoleza moyo na ari ya mchakato wa majadiliano ya kiekumene; kwa kufahamiana, kuheshimiana na kushirikiana kwa pamoja, ili majadiliano ya kiekumene katika maisha ya kitawa yawe kweli ni msaada mkubwa katika mchakato wa hija ya umoja wa Makanisa yote!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.