2015-01-19 11:36:43

Watanzania wanataka haki, amani na utulivu!


Serikali ya Tanzania inamshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kulipandisha Jimbo la Dodoma kuwa ni Jimbo kuu na hivyo kuupatia hadhi zaidi Mkoa wa Dodoma ambao ni Makao makuu ya Tanzania. Dodoma ni kati ya Majimbo makuu matano yanayounda Kanisa Katoliki la Tanzania. Jimbo hili lilitangazwa rasmi na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 6 Novemba 2014 na kumteua Askofu Beatus Kinyaiya kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dodoma.

Kuundwa kwa Jimbo kuu la Dodoma ni kielelezo makini cha kukua na kuimarika kwa imani na baraka kwa Familia ya Mungu Jimboni humo, changamoto ya kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo, umoja na mshikamano wa kitaifa, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wote!

Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Dr. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mara baada ya Ibada ya kumsimika Askofu mkuu Beatus Kinyaiya wa Jimbo kuu la Dodoma, Jumapili, tarehe 18 Januari 2015, kwenye Viwanja vya Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo kuu la Dodoma.

Serikali ya Tanzania inalishukuru na kulipongeza Kanisa Katoliki kwa mchango wake uliotukuka katika sekta ya elimu, afya na ustawi wa jamii na kwamba, limekuwa mstari wa mbele katika kuisaidia Serikali kupambana na umaskini, ujinga na maradhi maadui wakuu wa Tanzania. Kanisa limewekeza sana katika utunzaji bora wa mazingira, kama sehemu ya mchakato wa kuboresha maisha ya watanzania wote.

Makamu wa Rais ambaye alikuwa anashangiliwa na umati mkubwa inatokana na ufundi aliouonesha wa kunukuu vifungu vya Biblia, katika hoja zake na kwamba, Kanisa Katoliki nchini Tanzania ni sawa na tawi la mzabibu ambalo limeshikamana na Yesu Kristo anayeliwezesha kuzaa matunda mengi katika medani mbali mbali za maisha ya Watanzania. Mchango unaotolewa na madhehebu na dini mbali mbali nchini Tanzania ni mkubwa na kwamba, Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote katika mchakato wa maboresho ya maisha ya watanzania wengi!

Askofu mkuu Beatus Kinyaiya katika nembo yake kama Askofu mkuu anakazia amani na mshikamano; mambo ambayo Makamu wa Rais anasema ni msingi thabiti katika maendeleo na ustawi wa binadamu wote; changamoto kwa watanzania kuhakikisha kwamba, wanadumisha: haki, amani, upendo, umoja na mshikamano wa kitaifa na kukataa katu katu kutumbukizwa katika kishawishi cha udini, ukabila na umajimbo, mambo ambayo hayana tija wala mashiko kwa maendeleo na ustawi wa Watanzania: kiroho na kimwili.

Makamu wa Rais anasema, amani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayopaswa kulindwa na kutetewa na wananchi wote na wala si dhamana ya wanasiasa peke yao! Waamini wanahamasishwa kuwa ni wachamungu, kutafuta kwa bidii kuwa na amani na watu wote, huku wakichuchumilia utakatifu wa maisha, ili shina la uchungu lisije likachipua na kuwasumbua katika maisha yao. Watanzania waendelee kuombea amani pamoja na kuitetea, kwa kutambua kwamba, wao wote ni watoto wa Mwenyezi Mungu.

Makamu wa Rais amewakumbusha waamini wa dini mbali mbali nchini Tanzania kwamba, ni dhambi kubwa kukashfu dini au imani ya jiani zao. Na mtu yeyote anayefanya hivyo atambue kwamba, anavunja Katiba ya Nchi ambayo kimsingi ni sheria mama na atashughulikiwa na vyombo vya dola. Amani inajengeka na kustawi mahali penye upendo, huruma na msamaha; mahali ambapo ubinafsi, chuki na uhasama hauna nafasi katika mioyo ya watu; wananchi wajitahidi kuushinda ubaya kwa kutenda mema.

Makamu wa Rais anasema kwamba, chaguzi mbali mbali zitakazofanyika nchini Tanzania kwa Mwaka 2015 ni mwaliko kwa wananchi kufanya maamuzi sahihi, ili kuwachagua watu safi watakaoiongoza nchi; kwa kuangalia sifa kuu za kiongozi kuwa ni mtu anayetambua kwamba, uongozi ni huduma na wala si kwa vile mtu anajisikia kutaka kuingia madarakani kupitia kwa migongo ya wanyonge. Serikali imejipanga barabara kuhakikisha kwamba, amani na utulivu vinalindwa na kudumishwa, ili kuwapata viongozi watakaoshirikiana na wananchi kujiletea maendeleo yao wenyewe.

Na Rodrick Minja,
Dodoma, Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.