Rais Benigno Simeon wa Ufilippini katika hotuba yake ya kumkaribisha Baba Mtakatifu
Francisko nchini Ufilippini, ili aweze kuzungumza na viongozi wa Serikali na Wanadiplomasia,
Ikulu mjini Manila, Siku ya Ijumaa, tarehe 16 Januari 2015, amemshukuru na kumpongeza
kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko, kuwa ni sauti ya kinabii, inayowaunganisha
na kupyaisha maisha watu wote wenye mapenzi mema!
Rais Simeon anasema, Baba
Mtakatifu Francisko amekuwa ni mfano bora wa kuigwa katika kusimama kidete kulinda
na kuwatetea maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; ushuhuda unaojikita
katika uhalisia wa maisha yake. Rais amekumbushia shida na magumu aliyokumbana nayo
katika safari yake kama mwanasiasa, kiasi cha familia yake kutengwa na wengi wakati
wa utawala wa mabavu nchini Ufilippini.
Katika kinzani na magumu nchini Ufilippini,
wengi walinyamazishwa, ni viongozi wa Kanisa walioonesha ujasiri wa kukemea nyanyaso
na madhulumu dhidi ya wananchi wa Ufilippini; Wakleri wakaonesha kuwa kweli ni kielelezo
cha wachungaji wema; wakasimama kidete kulinda na kuimarisha imani ya Familia ya Mungu
nchini Ufilippini; wakajenga umoja na mshikamano wa kidugu, leo hii ni familia moja
inayowajibika na kutaabikiana katika raha na magumu ya maisha.
Rais Simeon
anasema, wanasiasa hawana budi kujikita katika mchakato wa kutafuta na kusimamia mafao
ya wengi ndani ya jamii, kila mtu akijitahidi kuwajibika na kamwe wasiwe ni watu wanaopandikiza
mbegu ya chuki na kinzani kati ya wananchi. Baba Mtakatifu katika hotuba yake kwa
wasaidizi wake wakuu alikuwa amekazia umuhimu wa kuondokana na tabia ya kufanya kazi
kwa mazoea na badala yake kujenga na kuimarisha moyo wa furaha katika huduma, ili
kujenga na kudumisha Ufalme wa Mungu hapa duniani.
Ni maneno ambayo Rais Simeon
anasema yanaonesha ujasiri wa Baba Mtakatifu katika ukweli na uwazi, changamoto hata
kwa wanasiasa kujivika ujasiri huu katika huduma kwa wanannchi wanaowahudumia. Serikali
ya Ufilippini katika mapambano ya kuleta mageuzi nchini humo, inatambua kwamba, kuna
kundi kubwa la watu ambalo linawaunga mkono, kumbe, si wapweke kamwe!
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.