2015-01-17 11:20:05

Dumisheni ukarimu kati ya watu!


Askofu msaidizi Daniel Adwok wa Jimbo kuu la Khartoum Sudan, ambaye hivi karibuni alitembelea katika maeneo ambayo bado yanawaka moto wa vita ya wenyewe kwa wenyewe Sudan ya Kusini, amekazia umuhimu wa majiundo makini kwa vijana wa kizazi kipya pamoja na kujenga moyo wa upendo na mshikamano kwa wakimbizi na wahamiaji, ambao wanatafuta hifadhi ya maisha yao badala ya kuwatelekeza.

Askofu msaidizi Adwork, akiwa katika maeneo haya, ameweza kukaa na kuzungumza na viongozi wa Serikali, viongozi wa Kanisa, wakimbizi na wahamiaji, ambao walimpokea kwa moyo wa shukrani kwa kuwasikiliza na kuwajali katika mahangaiko yao. Amewakumbusha wananchi wa Wilaya ya Maban ambao miaka kadhaa iliyopita walilazimika kuyakimbia makazi yao ili kutafuta hifadhi Kaskazini mwa Sudan au Nchini Ethiopia. Kumbe, kuna haja ya kujenga na kuimarisha utamaduni wa ukarimu kwa wakimbizi na wahamiaji. Wilaya ya Maban kwa sasa inatoa hifadhi kwa wakimbizi na wahamiaji wapatao 130, 000 kutoka Blue Nile.

Askofu msaidizi Adwok pia ametembelea na kukagua miradi mbali mbali inayoendeshwa na Shirika la Wayesuit kwa ajili ya kuwahudumia Wakimbizi, JRS kwa kukazia umuhimu kwa Mashirika ya misaada ya Kanisa Katoliki kuhakikisha kwamba, yanaangalia kwa makini mahitaji ya wakimbizi na wananchi mahalia, ili kujenga na kudumisha amani kati ya makundi haya mawili.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.