Shikamaneni na maskini ili kuwajengea imani na matumaini mapya!
Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 16 Januari 2015 ameadhimisha Ibada ya Misa
Takatifu kwa ajili ya Wakleri, Watawa na Majandokasisi kutoka nchini Ufilippini pamoja
na wawakilishi kutoka katika nchi mbali mbali Barani Asia, kwani hija hii ni kwa ajili
ya Bara la Asia katika ujumla wake. Ibada hii imefanyika kwenye Kanisa kuu la Bikira
Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, Jimbo kuu la Manila.
Katika mahubiri yake
kwa namna ya pekee kabisa Baba Mtakatifu ameitaka Familia ya Mungu nchini Ufilippini
kuonesha upendo wa dhati kwa Kristo pamoja na kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini,
kwani hawa ni hazina kubwa ya Injili. Amewakumbusha viongozi wa Kanisa pamoja na watawa
kwamba, ufuasi na upendo wao kwa Kristo unasaidia kukuza mchakato wa upatanisho.
Kama
sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 500 ya Ukristo nchini Ufilippini,
yatakayofikia hatima yake kunako mwaka 2021, Baba Mtakatifu anasema kwamba, kizazi
kilichopita kimesaidia kwa kiasi kikubwa watu kufahamu Neno la Mungu, tunu msingi
za maisha ya Kikristo, ambazo zimemwilishwa katika huduma ya mapendo, upatanisho,
mshikamano na mafao ya wengi. Tunu hizi zimeimarisha si tu wakati wa mahubiri au ujenzi
wa Kanisa nchini Ufilippini, bali pia zimesaidia kumwilisha Injili ya Upendo, msamaha,
mshikamano na huduma kwa ajili ya mafao ya wengi.
Baba Mtakatifu anawaalika
vijana wa kizazi kipya kuhakikisha kwamba, wanajenga madaraja yatakayolisaidia Bara
la Ulaya kupokea Neno la Mungu. Watu hawana budi kuonesha upendo kwa Kristo anayewaletea
upatanisho wa kweli. Mchakato wa kukutana na Yesu hauna budi kuwakirimia waamini wongofu
pamoja na kuchunguza dhamiri kama mtu binafsi na jamii katika ujumla wake. Injili
ya Kristo haina budi kusaidia mchakato wa ujenzi wa jamii imara inayojikita katika
msingi wa haki na kukombolewa.
Baba Mtakatifu anawapongeza Maaskofu Katoliki
nchini Ufilippini wanaosimama kidete kupambana kufa na kupona na mambo yanayosababisha
ukosefu wa haki na usawa katika jamii. Injili inamchangamotisha kila mwamini kuhakikisha
kwamba, anaishi kwa kuzingatia misingi ya uaminifu, ukweli pamoja na kujisadaka kwa
ajili ya mafao ya wengi. Injili inawataka Wakristo kujenga na kudumisha makundi ya
watu waaminifu; wenye kushikamana pamoja na kujitoa kwa ajili ya kuleta mageuzi ndani
ya jamii kwa njia ya ushuhuda wa kinabii.
Baba Mtakatifu Francisko kwa kuiangalia
changamoto hii, anawataka kwa namna ya pekee, Wakleri na watawa kujenga utamaduni
wa kusali kila siku kama sehemu ya mchakato wa kukutana na Kristo pamoja na kupambana
kufa na kupona, ili kukataa kishawishi cha kutaka kumezwa na malimwengu; ubinafsi
pamoja na kupenda mali badala yake, wawe ni watu wanaojisadaka kwa ajili ya ustawi
na maendeleo ya jirani zao; watu wakweli na waaminifu; wanaosaidia ustawi na maendeleo
ya mtu mzima: kiroho na kimwili; tayari kujitosa kimasomaso kwa ajili ya kueneza Injili
katika jamii inayojikita kwenye ubaguzi, mvuto usiokuwa na mashiko pamoja na kashfa
ya ukosefu wa misingi ya usawa.
Baba Mtakatifu anawataka Maaskofu kutoa kipaumbele
cha pekee kwa Mapadre vijana, watawa na majandokasisi, ambao walikuwa wamefurika kwa
wingi katika Ibada hii ya Misa Takatifu, wanaoweza kuchanganyikiwa n akukata tamaa,
lakini bado wanaendelea kuliona Kanisa kama mwenzi katika hija ya maisha yao na chemchemi
ya furaha. Kanisa linapaswa kuwa karibu zaidi na wale wote wanaoelemewa na umaskini,
rushwa na ufisadi, kiasi cha kujikatia tamaa, kiasi hata cha kuingiwa na kishawishi
cha kuacha masomo na kujitosa barabarani.
Baba Mtakatifu anawataka Wakleri
kutangaza uzuri na ukweli wa ndoa ya Kikristo katika jamii ambamo kuna mambo mengi
ambayo yanaendelea kuwachanganya watu kuhusiana na maisha ya ndoa na familia. Huu
ni ukweli ambao unakabiliwa na changamoto nyingi, zinazotaka kuathiri mpango wa kazi
ya uumbaji na kupotosha ukweli wa tunu msingi za maisha zilizounda na kujenga uzuri
wa utamaduni wa Ufilippini.
Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha mahubiri
yake kwa Wakleri, Watawa na Majandokasisi kwa kusema kwamba, miaka 500 ya Ukristo
nchini humo si haba, kwani imesaidia kujenga upendo mkubwa kwa Mwenyezi Mungu, Ibada
kwa Bikira Maria na Rozari Takatifu, muhtasari wa Injili. Hapa kuna nguvu kubwa inayoweza
kusaidia mchakato wa umissionari unaopaswa kusaidia utamaduni wa Kikristo miongoni
mwa vijana wa kizazi kipya, ili ari na moyo wa Kikristo uweze kupenya na hatimatimaye
kuota mizizi katika jamii ya Wafilippini na kwa njia yao, jamii nyingine sehemu mbali
mbali za dunia.
Naye Kardinali Luis Antonio Tagle, Askofu mkuu wa Jimbo kuu
la Manila katika hotuba yake ya kumkaribisha Baba Mtakatifu kuadhimisha Fumbo la Ekaristi
Takatifu, ametambua uwepo wa uwakilishi wa Familia ya Mungu kutoka Barani Asia. Kanisa
kuu la Manila ni kielelezo makini cha wananchi wa Ufilippini, Kanisa ambalo limekumbana
na majanga mbali mbali katika historia, lakini bado liko imara; Pande zote twadhikika,
bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa. Furaha ya wananchi wa Ufilippini
inajikita katika muziki na imani inayowawezesha kusimama tena na kusonga mbele baada
kukumbwa na majanga mbali mbali katika maisha.
Kardinali Luis Antonio anasema,
uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko kati yao ili kuwaletea moto unaowatakasa; tetemeko
linalowaamsha, anawaletea silaha ili kuwalinda na kuendelea kulijenga Kanisa la Kristo
sanjari na kuwaimrisha ndugu zake katika imani, matumaini na mapendo.
Mara
tu baada ya Ibada ya Misa Takatifu, Papa Francisko amekwenda kuwatembelea na kuwaslimia
watoto wanaoishi katika mazingira magumu wanaotunzwa na Kituo cha TNK kilichoanzishwa
na Padre Mathieu. Baba Mtakatifu amezungumza na watoto hawa, akapiga nao picha za
kumbu kumbu na baadaye wakampatia zawadi ya Sanamu ya Bikira Maria na zawadi nyingine,
mwishoni, anasema Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican, Baba Mtakatifu
akawabariki na hatimaye kuendelea na ratiba yake.
Na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.