2015-01-15 07:46:54

"Sisi sote ni Wanaigeria"


Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, Alhamisi tarehe 15 Januari 2015 inawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushikamana kwa njia ya sala kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea watu ambao wanaendelea kupoteza maisha yao nchini Nigeria kutokana na mashambulizi ya kigaidi, ambayo kwa sasa yameingia katika mtindo wa hatari kwa kutumia watoto wadogo wanaojitoa mhanga ili kuwaangamiza ndugu zao.

Ibada hii ya sala inatarajiwa kuongozwa na Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la familia, kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria in Trastevere, mjini Roma. Takwimu zinaonesha kwamba, zaidi ya watu elfu mbili wameuwawa kikatili kutokana na mashambulizi ya kikundi cha kigaidi cha Boko Haram na kwamba, kuna umati mkubwa wa watu ambao umelazimika kuyakimbia makazi yake kwa kuhofia usalama wa maisha.

Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, Jumapili iliyopita imeshiriki pia katika maandamano ya amani mjini Paris, Ufaransa, kupinga vitendo vya kigaidi vinavyotishia umoja na utofauti wa wananchi wa Ulaya pamoja na juhudi za kuimarisha uhuru wa kujieleza. Lakini, Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao makuu mjini Roma na ambayo imekuwa mstari wa mbele katika mchakato wa upatanisho sehemu mbali mbali za dunia, imeikumbusha Jumuiya ya Kimataifa kwamba, kuna watu wasiokuwa na hatia nchini Nigeria wanaendelea kupoteza maisha yao kutokana na vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Boko Haram, kumbe hata Nigeria inapaswa kuungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa kama ilivyofanya kwa Ufaransa iliposhambuliwa na magaidi hivi karibuni.

Mkutano huu wa sala unaongozwa na kauli mbiu "Sisi sote ni Wanaigeria". Mashambulizi ya kigaidi nchini Nigeria hayabagui wala kuchagua, kumbe, kuna haja ya kuonesha mshikamano wa dhati kwani kuna umati mkubwa wa waamini wa dini ya Kiislam ambao unajikita katika majadiliano, maridhiano na amani katika ya watu. Kundi hili linapaswa kuungwa mkono, ili kweli dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi kwa kuheshimiana na kuthaminiana kama ndugu na kwamba, tofauti za kidini zisiwe ni chanzo cha karaha na maafa kati ya watu.

Waamini na watu wenye mapenzi mema wanasali kwa ajili ya kuombea mchakato wa ushirikishwaji wa wahamiaji na wageni uendelee kwa kuzingatia misingi ya utu na heshima ya binadamu. Kusiwepo tena mtu au kundi la watu linalojihusisha na mashambulizi ya kigaidi kwa kisingizio cha kidini. Jumuiya ya Mtakatifu Egidio inapenda kuikumbusha Jumuiya ya Kimataifa hatari kubwa iliyoko nchini Nigeria na nchi ambazo ziko katika Ukanda wa Sahara zinavyotishiwa usalama, ustawi na maendeleo yake kutokana na vitendo vya kigaidi.







All the contents on this site are copyrighted ©.